Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 00:56

Ulaya yarejea katika masharti ya watu kusalia nyumbani kutokana na wimbi la pili la maambukizi ya Corona


Hisa katika masoko makubwa duniani zimeanguka kufuatia ripoti kwamba nchi zenye uchumi mkubwa duniani zimerudisha masharti ya watu kusalia nyumbani kama ilivyokuwa awali na kupelekea uchumi wa dunia kudorora.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron na Kansela wa ujerumani Angela Merkel wameziamuru nchi zao kurejesha kwa tena amri ya watu kusalia nyumbani kwao kudhibithi wimbi la pili la maambukizi ya virusi vya Corona yanayotishia nchi za ulaya.

Hisa katika masoko makubwa duniani zimeanguka kufuatia ripoti kwamba nchi zenye uchumi mkubwa duniani zimerudisha masharti ya watu kusalia nyumbani kama ilivyokuwa awali na kupelekea uchumi wa dunia kudorora.

Macron amesema kwamba “virusi vya Corona vinasambaa kwa kasi sana kuliko ilivyotabiriwa na kwamba wamezidiwa na kasi ya virusi hivyo.”

Ameendelea kusema kwamba “virusi vya Corona vinaendelea kusababisha madhara makubwa na huenda hali ikawa mbaya zaidi ya ilivyokuwa wakati wa wimbi la kwanza.”

Serikali ya Ufaransa imewataka watu kusalia nyumbani na kuruhusiwa tu kutoka nje iwapo wanaenda kununua bidhaa muhimu, kutafuta huduma za afya, au kufanya mazoezi.

Wafanyakazi pia wanaruhusiwa kwenda kazini iwapo mwajiri wao anaonelea kwamba lazima wafike kazini na kazi hiyo haiwezi kufanywa wakiwa nyumbani.

Hata hivyo, shule zitaendelea kufunguliwa.

Kila mtu anayeondoka nyumbani kwake atahitajika kubeba kibali kutoka kwa mamlaka, kuonyesha sababu yake ya kuwa nje.

Ujerumani imetangaza kufunga baa, migahawa na majumba ya Sanaa kuanzia Novemba 2 hadi 30.

Wanafunzi wataendelea kwenda shuleni nchini Ujerumani huku maduka yakifunguliwa kwa kuzingatia masharti makali.

Wakati huo huo, rais wa tume ya umoja wa ulaya Ursula Von der Leyen amesema kwamba umoja huo utatumia dola millioni 117 kwa ajili ya kufanya vipimo vya haraka vya covid 19, wakati virusi hivyo vinaongezeka kwa kasi kote barani ulaya.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Brussels, Von der Leyen amesema kwamba “kila nchi ya ulaya inahisi athari za wimbi la pili la virusi vya corona.”

Kituo cha umoja wa ulaya cha kukinga na kudhibiti magonjwa, kimesema kwaba virusi vya corona vinaendelea kuenea kote barani ulaya.

Kituo hicho kimeripoti kuwa watu millioni 6 na laki 5 wameambukizwa virusi vya corona katika nchi wanachama wa umoja wa ulaya, ukijumulisha Uingereza, Iceland, Liechtenstein, Norway na Uswizi.

Wataalamu wa afya barani ulaya wanasema virusi hivyo vinasambaa kwa haraka, na hawawezi kutegemea vipimo vinavyochukua siku nzima ndipo aliyepimwa ajue matokeo.

Imetayarishwa na Kennes Bwire na Patrick Nduwimana, VOA, Washington DC

XS
SM
MD
LG