Kenyatta aliwasili muda mfupi kabla ya saa sita na kushangiliwa na wapiga kura waliokuwa wamepanga foleni wakisubiri kushiriki katika zoezi hilo.
Punde tu baada ya kupiga kura, Kenyatta aliwahutubia waandishi wa habari - wakiwemo wale wa kimataifa - waliokuwa wanasongamana ili kupata kauli kutoka kwake.
Mwanasiasa huyo, ambaye anawania urais kwa mara ya tatu, aliiambia Sauti ya Amerika kwamba alikuwa na imani ya kupata ushindi mkubwa dhidi ya mpinzani wake mkuu, kiongozi wa chama cha ODM, Raila Odinga, ambaye anawania akiwakilisha muungano wa National Super Alliance (NASA).
Alisisitiza ujumbe wake alioutoa kwenye hotuba ya kufunga kampeni kwamba baada ya Wakenya kupiga kura, ni heri warudi nyumbani na kusubiri matokeo.
Odinga alipiga kura mwendo wa saa tano na Nusu katika eneo la uwakilishi bunge la Kibra, nje kidogo ya mji wa Nairobi. Mwanasiasa huyo mwenye umri wa miaka 72 alisema anamatumaini kwamba Wakenya watampa fursa ya kushika usukani kama rais wa tano.