Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 00:18

Maafisa wa Uganda na Rwanda Washindwa Kufikia Muafaka


Rais Paul Kagame wa Rwanda na Rais Yoeri Museveni wa Uganda, wakipeana mikono baadayakutia saini Mkataba wa Rwanda na Uganda.
Rais Paul Kagame wa Rwanda na Rais Yoeri Museveni wa Uganda, wakipeana mikono baadayakutia saini Mkataba wa Rwanda na Uganda.

Maafisa wa Uganda na Rwanda wameshindwa kufikia makubaliano katika masuala makuu muhimu baada ya mkutano wa faragha wa takriban saa nane uliofanyika mjini Kampala.

Masuala hayo ambayo yameshindwa kutatuliwa na maafisa hao hivi sasa yatapelekwa kwa wakuu wa mataifa hayo mawili, Rais Yoweri Museveni wa Uganda na rais wa Rwanda, Paul Kagame ili kupatiwa ufumbuzi.

Ajenga ya mkutano wa Kampala ilikuwa imepangwa awali. Maafisa walikuwa wakijadili masuala ambayo yanahusu shutuma za kudumaza uthabiti na hatua ambazo zimechukuliwa, na kulinda haki na uhuru wa wananchi wa mataifa hayo na kuanzisha harakati za kibiashara kwenye eneo la mpaka kati ya Uganda na Rwanda.

Hata hivyo mkutano huo umeshindwa kufikia muafaka.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda, Olivier Nduhungirehe aliorodheshan mambo ambayo Rwanda inaamini ni kiini kwa mzozo wa nchi hizo.

“Makundi yenye silaha yamekuwa yakifanyia operesheni zao nchini Uganda na kupatiwa msaada. Tumejadili na kuwapatia habari muhimu, tumewapa na majina. Pia tumezungumzia suala la wanyarwanda ambao wanakamatwa kiholela na kinyume na sheria wanawekwa kizuiini na pia kuteswa katika nchi hii,” amesema waziri Nduhungirehe.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uganda, Sam Kutesa amejibu masuala muhimu ambayo nchi yake inayasisitiza yanahitaji suluhisho la Rwanda na wakati huko kukana baadhi ya shutuma zilizotolewa na waziri wa Rwanda.

“Masuala kama majaribio ya kujiingiza katika idara zetu za usalama. Masuala kama kufunguwa kwa mpaka hatua iliyochukuliwa na Rwanda. Pia tumezungumzia kuhus wanyarwanda ambao wamekuwa wakikamatwa hapa kutokana na harakati ambazo ni kinyume cha sheria na baadhi yao wamefukuzwa nchini. Kwa Uganda, kwa kwweli, hatujawahi kuliunga mkono kundi lolote lenye silaha wala kudumaza uthabiti au kuwa na azma ya kuyumbisha uthabiti wa taifa jirani ikiwemo Rwanda,” amesema waziri Kutesa.

Wakati Rwanda imeelezea matumaini yake kwamba masuala haya yanawezwa kusuluhishwa kwa nia njema, Uganda imesema ina matumaini kwa ukweli na uaminifu.

Marais wa Rwanda na Uganda walitia saini waraka wa maelewano mwezi Agosti nchini Angola ambapo walikubaliana kufanya kazi katika kupatikana kwa sitisho la mgogoro uliopo kwenye mpaka baina ya mataifa hayo mawili.

Mkutano wa Jumamosi ulisimamiwa na maafisa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo na Angola ukiongozwa na waziri wa Mambo ya Nje wa Angola, Manuel Domingos Augusto ambaye alikuwa na matumaini mgogoro huo utasuluhishwa.

Mawaziri wa mambo ya nje wamekubali kuwasilisha masuala hayo kwa rais wa Uganda Yoweri Museveni na rais wa Rwanda Paul Kagame ili kuamua jinsi ya kusonga mbele.

XS
SM
MD
LG