Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Aprili 23, 2024 Local time: 09:03

Uganda, India zaendeleza uhusiano wao


Waziri Mkuu wa India Narendra Modi akipokelewa na mwenyeji wake Rais Yoweri Museveni wa Uganda
Waziri Mkuu wa India Narendra Modi akipokelewa na mwenyeji wake Rais Yoweri Museveni wa Uganda

Uganda imeboresha uhusiano wake na India, miongo miwli baada ya raia wa India kufukuzwa nchini humo na kutaifishwa biashara zao.

Katika ziara yake ambayo imepewa umaarufu mkubwa nchini Uganda, Waziri Mkuu wa India Narendra Modi alipewa fursa pekee ya kwanza kwa kiongozi wa India kuhutubia bunge la Uganda.

Waziri Mkuu ametangaza kutoa mkopo wa dola milioni 200 kwa Uganda. Ameeleza kuwa mkopo huo utaiwezesha Uganda kununua vifaa muhimu vya matibabu hasa kwa tiba ya ugonjwa wa saratani, vifaa vya nishati, teknohama, filamu na kilimo, na dola 929,705 zitakwenda katika maendeleo ya miradi ya pamoja kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

"Dola milioni 200 zinawasubiri kwa matumizi yenu ili kuwanufaisha raia wa Uganda na tunaahidi msaada zaidi wa kijeshi na maswala mengine ya maendeleo," amesema Modi.

Pia India na Uganda zimekubaliana kuwaruhusu raia wa nchi hizo mbili wenye pasipoti za kidiplomasia, kusafiri baina ya nchi hizo bila visa.

Rais wa Uganda amesema kwamba safari ya kwanza ya shirika la ndege la Uganda ambalo linapanga kufufua safari zake ifikapo Januari 2019, itakuwa kuelekea nchini India ili kuimarisha sekta ya utalii ya Uganda na biashara.

Rais Yoweri Museveni amesema:Tunafufua safari zetu za ndege ya Uganda airlines na ninamuomba waziri mkuu Modi kukubali safari yetu ya kwanza kuwa ya kuelekea India. Sitaki kwenda kwingine ambapo sijui. Najua vizuri kwamba watu wa ukoo wangu wanatoka India na huko ndiko nitaenda.

Idadi ya raia wa India nchini Uganda ni ndogo sana, chini ya asilimia moja ya idadi ya watu nchini humo.

Idadi kubwa ya viwanda na biashara nchini Uganda, vinamilikiwa na raia wa India na wanachangia asilimia 65 ya ushuru wa Uganda. Wakati walipofurushwa mnamo mwaka 1972, raia wa India walikuwa wanamiliki asilimia 90 ya biashara za Uganda na kuchangia kwa pato la taifa kwa kiwango cha asilimia 90.

Kulingana na hesabu za benki kuu ya Uganda, Uganda imetumia kiasi cha dola milioni 774 kununua bidhaa kutoka nchini India, mwaka 2017.

Imetayarishwa na Mwandishi wetu Kennes Bwire, Washington, DC.

XS
SM
MD
LG