Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 04:29

Uchaguzi Kenya utaendelea tarehe 26 kama ilivyopangwa - IEBC


Afisa mkuu mtendaji wa IEBC, Ezra Chiloba.
Afisa mkuu mtendaji wa IEBC, Ezra Chiloba.

Tume ya uchaguzi na mipaka ya Kenya, IEBC, ilitangaza Jumatano jioni kwamba uchaguzi wa urais wa marudio utafanyika tarehe 26 mwezi huu kama tu ilivyopangwa.

Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na tume hiyo ilisema kuwa wagombea wote wanane walioshiriki kwenye uchaguzi uliobatilishwa wa tarehe 8 mwezi Agosti wako huru kushiriki katika zoezi hilo.

Tume hiyo ilisema kuwa itachapisha majina ya wagombea wote kwenye gazeti rasmi la serikali, kama ilivyoariwa na mahakama hiyo.

Haya yalijiri siku moja baada ya mgombea wa muungano wa upinzani, Raila Odinga, kutangaza kwamba amejitoa kwenye kinyang'anyiro hicho.

Rais Uhuru Kenyatta alisema Jumanne kuwa ataendelea na kampeni zake na kuwarai wafuasi wake kujitokeza kwa wingi mnamo siku hiyo ya uchaguzi.

Mapema Jumatano, mahakama kuu mjini Nairobi iliamuru kwamba aliyekuwa mgombea wa urais kwa tikiti ya chama cha Thirdway Alliance, Ekuru Aukot, aruhusiwe kushiriki kwenye uchaguzi huo wa marudio.

Punde tu baada ya Odinga kutangaza hatua hiyo, mjadala mkubwa uliibuka kuhusu hatua za kisheria zilizofaa kufuata kutatua mgogoro huo wa kisiasa na kuepusha nchi hiyo ya Afrika Mashariki kutumbukia kwenye mzozo wa kikatiba.

"Hii ni hali ambayo haijawahi kushuhudiwa katika historia ya Kenya na kuna njia kadhaa za kuzuia mzozo wa kikatiba iwapo wagombea wataamua kujiondoa kabla ya siku ya uchaguzi," mwanasheria Bob Mkangi - ambaye ni mmoja wa mawakili waliotayarisha rasimu ya katiba ya Kenya ya mwaka wa 2010 - aliiambia idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika kwa njia ya simu.

Siku kumi na nne baada ya uchaguzi mkuu kufanyika, mahakama ya juu ilifuta matokeo ya uchaguzi wa rais yaliyokuwa yametangazwa na IEBC na kuipa tume hiyo siku 60 kufanya uchaguzi mpya kwa mujibu wa katiba.

Majaji wanne wa mahakama hiyo wakiongozwa na jaji mkuu David Maraga walisema kwenye uamuzi wao kwamba uchaguzi huo uligubikwa na dosari na ukiukaji wa sheria.

Hata hivyo, majaji wawili wa mahakama ya juu hawakukubiliana na uamuzi huo.

Baada ya uamuzi huo, NASA iliwasilisha orodha masharti kumi na moja ambayo ilisema ni lazima yatimizwe kabla ya mgombea wao kukubali kushiriki katika uchaguzi huo.

Polisi warusha gesi ya kutoa machozi kuwatawanya waandamaji mjini Nairobi.
Polisi warusha gesi ya kutoa machozi kuwatawanya waandamaji mjini Nairobi.

Baadaye NASA iliwauliza wafuasi wake kufanya maandamano katika miji mbalmbali kuishinikiza IEBC kutimiza matakwa hayo.

Maandamano yamekuwa yakifanyika katika miji kama vile Nairobi, Kisumu na mombasa huku kukiriporitiwa visa kadhaa vya vurugu, ghasia na makabiliano na maafisa wa kulinda usalama.

Akitangaza kujiondoa kwenye kinyang'anyiro hicho, Odinga aliwataka wafuasi wake kwendelea na maandamano.

"Hakuna uchaguzi utaendelea bila mageuzi kufanyika kwa IEBC," alisema mwanasiasa huyo.

XS
SM
MD
LG