Mgombea wa urais wa chama cha Republikan wa Marekani Donald Trump, siku ya Jumatatu ametoa wito wa kuwepo na sera za mambo ya nje ambazo zinatilia maanani ukweli wa mambo na ambazo zinalenga kuliangamiza kundi la kigaidi la Islamic State na makundi mengine yenye itikadi kali, badala ya kile alichokiita kubadilisha utawala ili kufuata maadili ya Marekani.
Akitoa hotuba yake juu ya sera za uhamiaji katika jimbo lenye ushindani mkubwa la Ohio, Trump alisema kuwa Marekani inahitaji kushirikiana na mataifa yote ambayo yanataka kushinda itikadi kali au ugaidi wa Kiislamu.
Wakati huo huo, mpinzani wa Trump wa chama cha Damokratik, Hillary Clinton, aliungana na makamu wa rais Joe Biden na kuhutubia mkutano wa kampeni katika mji wa Scranton, jimbo la Pennsylvania. Biden, ambaye alikuwa anafanya mkutano wa kwanza wa hadhara na Clinton, alisisitiza msimamo wake wa awali kwamba Trump ana mapungufu mengi na kwamba haahitimu kuongoza nchi kama Marekani.