Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 14:58

Trump arejea katika kampeni wakati Biden anaelekea majimbo yenye ushindani


Rais Donald Trump, kushoto, na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.
Rais Donald Trump, kushoto, na Makamu wa Rais wa zamani Joe Biden.

Rais Donald Trump anarudi kwenye uwanja wa kampeni Jumatatu baada ya kuugua ugonjwa wa COVID-19 huku mpinzani wake makamu rais wa zamani Joe Biden akielekea katika majimbo yenye ushindani kabla ya uchaguzi mkuu wa Novemba 3.

Wakati huo huo kamati ya sheria ya Baraza la Seneti linaanza Jumatatu kusikiliza Ushahidi wa Amy Coney Barrett aliyechaguliwa na Trump kuchukua nafasi katika mahakama ya juu ya taifa.

Baraza la Seneti limesitisha kazi zake kutokana na maseneta kadhaa kuambukizwa na virusi vya corona, lakini Warepublican wanakataa kuchelewesha kuidhinishwa kwa Jaji Barrett kuchukua nafasi katika mahakama ya juu.

Wao wanataka kumuidhinisha kabla siku ya uchaguzi Novemba 3. Na hata wanafanya mipango maalum kuwaruhusu Maseneta wanaougua COVID-19 kuweza kuingia bungeni kupiga kura, huku Wademokrats wakionekana kushindwa kuzuia utaratibu huo.

Hayo yakiendelea ikiwa imebaki wiki tatu kabla ya siku ya uchaguzi wa rais, Trump amesema mwishoni mwa wki kwamba yuko tayari kurudi kwenye kampeni baada ya kupona kutokana na ugonjwa wa COVID-19.

Donald Trump amesema : "Cha kwanza kabisa, ninajisikia vyema. Sijui nyinyi mnajihisi vipi. Mukoje hapo? Niko tayari kuanza kampeni."

Daktari wake alitoa taarifa jana Jumapili akisema kwamba rais mgombea wa chama cha Republican hachukuliwe tena kama mtu aneweza kuambukiza mtu.

Lakini mdahalo wa wagombea kiti cha rais uliopangwa kufanyika wiki hii umefutwa baada ya Trump kukataa kushiriki kupitia mtandao na mpinzani wake Joe Biden.

Akizungumza katika kipindi cha This week cha kituo cha televisheni cha ABC Eric Trump alitetea uamuzi wa baba yake akisema wagombea hukutana ana kwa ana.

Eric anafafanua : "Hivyo ndivyo namna midahalo imekuwa ikifanyika Marekani kwa angalau miaka 200 iliyopita. Unasimama na kujadiliana na mtu mwengine. Na babangu hataki kufanya kupitia mawasiliano ya simu. Anataka kusimama kwenye jukwa kumtizama mtu usoni na Biden hayuko tayari kufanya hivyo.

Kampeni ya Biden inasema mgombea wao yuko tayari kujadilianana Trump ana kwa ana hapo Oktoba 22, almuradi tu rais amepona na hawezi kumuambukiza mtu tena baada ya kuugua Covid 19.

Biden akiwa anaongoza kwa aili mia 12 kufuatana na utafiti wa maoni wa kitaifa uliofanyika hivi karibuni anaelekea katika jimbo la Ohio leo mojawapo ya majimbo yenye ushindani.

Naye Trump wiki hii amepanga kurudi Florida na baadae Pennsylvania majimbo mawili ambayo lazima ushinde ili kuweza kunyakuwa ushindi wa kiti cha rais.

Kampeni zikiwa zinaendelea watu katika majimbo mengi wanaendelea kupiga kura.

Gazeti la New York Times linaripoti kwamba idadi ya watu waliojitokeza katika jimbo la Wisconsin ni kubwa sana.

Katika wilaya ya Dane ngome ya Wademokrats katika jimbo hilo idadi ya kura kwa njia za posta zilizokwisha rudishwa tayari ni zaidi ya asilimia 36 ya idadi ya jumla zilizofikishwa wakati wa uchaguzi wa 2016.

Mwenyekiti mwenza wa kampeni ya Biden, Cedric Richmond anasema wanawaambia watu kupiga kura zao mapema katika majimbo yanayowaruhusu.

Richmond anaeleza : "Tunawaambia watu kutumia nafasi hii ya kuweza kupiga kura mapema katika baadhi ya majimbo. Na kumbuka mimi nina gombania kiti huko New Orleans na jimbo la Lousiana limeanza upigaji kura mapema tangu jana. Na ninawahimiza wapiga kura kutumia nafasi hii ya upigaji kura wa mapema Ikiwa ni njia nzuri kabisa kupunguza mistari mirefu ya watu siku ya uchaguzi."

Wasiwasi mkubwa wa kampeni ya Rais Trump ni kwamba kawaida ni wapigaji kura wa chama cha Demokratik wanapiga kura zaidi kwa njia ya posta, na wachambuzi wanadai huenda ndio maana Rais Trump analalamika kuwepo udanganyifu kutokana na uchaguzi kupitia posta.

XS
SM
MD
LG