Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 07:27

Tanzania yatarajiwa kuwasilisha hoja bungeni ya kulinda taarifa binafsi


Waziri Nape Nnauye.
Waziri Nape Nnauye.

Tanzania inatarajiwa kuwasilisha Bungeni hoja itakayopelekea  kuwepo sheria zitakazolinda taarifa binafsi za mwananchi ili kuhakikisha sekta ya mtandao inakuwa salama.

Kwa mujibu wa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye, hatua hiyo inafuatia Baraza la Mawaziri kuridhia kutungwa sheria, hoja hiyo inatarajiwa kuwasilishwa katika kikao kijacho cha Bunge kinachoanza Jumanne ijayo Septemba 13 mwaka 2022.

Waziri Nape ameyasema hayo jijini Dar es Salaa katika kongamano lililowakutanisha wadau wa TEHAMA wakiwemo wa miundo mbinu kutoka ndani na nje ya Tanzania, akiwataka wadau kutoa maoni huru yatakayopelekwa Bungeni na kujadiliwa ili sheria itakayotungwa iwe bora na yenye kulinda taarifa binafsi za Watanzania.

Aidha Waziri Nape amesema kongamano hilo limetoa taswira chanya kwa Tanzania katika ramani ya dunia hususani kwenye mabadiliko ya Teknolojia kwa lengo la kujenga uchumi wa kidigitali na kutatua changamoto za kimawasiliano huku akibainisha dhamira ya serikali kuhakikisha hakuna mwananchi anayeachwa nyuma katika fursa zinazotokana na masuala ya teknolojia.

Baadhi ya Watanzania wamekuwa wakikumbana na changamoto katika kulinda usiri kwenye utoaji wa taarifa mbalimbali hususan kwenye mitandao huku watu kadhaa wakiwa tayari wamekumbana na kadhia ya kuingia katika utata wa kisheria juu ya suala hilo.

XS
SM
MD
LG