Rais Jakaya Kikwete anamaliza muda wake wa uongozi baada ya kuongoza nchi hiyo kwa awamu mbili za miaka mitano mitano tangu 1995. Katiba ya Tanzania haimruhusu Rais kuwania uongozi kwa awamu ya tatu.
Ushindani wa kisiasa ni mkali sana katika uchaguzi wa jamhuri ya muungano kati ya vyama viwili vikuu, chama tawala cha CCM ambacho kimemuweka Dr. John Pombe Magufuli kuwania urais na chama cha upinzani cha Chadema, ambacho ni mwamvuli wa umoja wa katiba ya wananchi – UKAWA – kimemteua waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa.
Vyama vingine vilivyo chini ya mwamvuli wa Ukawa ni pamoja na CUF, NCCR-Mageuzi. Chama cha ACT ambacho kinaongozwa na mwanasiasa aliyejitenga na Chadema, Zitto Kabwe, nacho kimemuweka Bi Anna Mghwira kuwania nafasi ya urais.
Uchaguzi huo pia unahusisha urais wa visiwa vya Zanzibar ambako Rais wa sasa Mohammed Shein wa chama tawala cha CCM anakabiliwa na upinzani mkali kutoka kwa Maalim Seif Shariff Hamad anayewakilisha chama cha muda mrefu wa upinzani, CUF.
Viti 265 katika bunge la jamhuri ya muungano ndio ambavyo vinagombaniwa katika majimbo (bara na visiwani) kuingia kwenye bunge litakalokuwa na jumla ya wabunge 486 – viti 221 vinatokana na uteuzi wa rais na makundi mbali mbali nchini humo. Kwa upande wa Zanzibar viti vinavyogombaniwa katika majimbo kuingia baraza la wawakilishi ni 54 ambalo litakuwa na jumla ya wawakilishi 86 – 32 wakiwa wanatokana na uteuzi wa rais na makundi mbali mbali visiwani humo.