Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 20:35

Tanzania: Wadau waishauri serikali kupitia upya rasimu ya mitaala ya elimu


Wanafunzi walikuwa ni moja ya wadau walioshiriki kutoa maoni kwenye rasimu ya sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023.
Wanafunzi walikuwa ni moja ya wadau walioshiriki kutoa maoni kwenye rasimu ya sera ya elimu na mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023.

Watafiti na wadau mbalimbali wa masuala ya elimu wameishauri serikali ya Tanzania kupitia upya rasimu ya mitaala ya elimu iliyotolewa Mei 2023 na kufanya marekebisho katika  baadhi ya sera ambazo zinaonekana kutokuwa sawa kabla ya kuanza kwa utekelezaji wake.

Wanaitaka serikali itamke wazi namna ya kuwasaidia wanafunzi pale inapotokea changamoto kwa ngazi zote za elimu.

Tangu rasimu ya sera ya elimu na mitaala itoke wadau mbalimbali wameonekana kutoridhishwa na baadhi ya mapendekezo katika rasimu hiyo huku wengine wakidai kuwa kuna mambo muhimu hayajazingatiwa katika kufikia kuiboresha elimu ya Tanzania

Akizungumza na Sauti ya Amerika Gryson Mgoi ambaye ni msimamizi kitengo cha mawasiliano katika shirika lisilo la kiserikali linalo jishughulisha na masuala ya elimu la Uwezo amesema licha ya Serikali kutamka mwanafunzi aliyepata uja uzito anaweza kurudi shule lakini rasimu ya sera haijazungumzia chochote kuhusu utaratibu wa kurudi shule.

Mgoi anasema kuwa:"Ilitiliwa mkazo sana kwenye sera nilitegemea liwepo ingawa limetolewa waraka hivi karibuni hili la mtoto wa kike kurudi shule akipata ujauzito. Lakini ili kulipa uzito nilitegemea itamkwe kwenye sera sasa watoto wa kike watapaswa kurudi shule na ielezwe vizuri kuhusu utaratibu wa kurudi, hilo nimeona limekosekana."

Kwa upande wake Katibu Mkuu kutoka chama cha watu wenye kuishi na ulemavu, SHIVYAWATA, Jonas Lubago amezitaka kamati zinazoendelea kuchambua sera kuitambua elimu jumuishi iwe ni hoja katika mapendekezo ya sera mpya huku watu wenye ulemavu zaidi ya mmoja (ambatano) watolewe tamko la wazi juu ya namna ya kuwafundisha.

Baadhi ya wataalam walio kongamana la sera na mitaala ya elimu Dodoma, Tanzania.
Baadhi ya wataalam walio kongamana la sera na mitaala ya elimu Dodoma, Tanzania.

Lubago anasema: “Sasa hivi wanahoja saba za sera ila tunatamani elimu jumuishi iwe ni hoja ya nane ndio tuiwekee matamko yake moja kwa moja ni kwanini tunasema hivyo kuna watu wenye kuishi na ulemavu ambatano kwenye matamko ya sera pale hakuna kitu kama hicho kinacho zungumzia mwenye kuishi na ulemavu zaidi ya mmoja atafundishwaje kwa mfano kiziwi, asiye ona atafundishwaje na mwalimu kwa idadi ya wanafunzi haijazungumzwa kwa sababu yule ni mwanafunzi mmoja anahitaji mwalimu mmoja.

Hata hivyo Michael Kamukulu ambaye ni mtafiti wa masuala ya elimu nchini ameishauri serikali kuangalia mfumo wa motisha katika rasimu ya sera waliouweka kwa kuhakikisha motisha unatolewa baada ya kuonekana matokeo na mabadiliko.

Kamukulu anaeleza: “Mfumo wa motisha inabidi uzingatiwe pia bahati nzuri tumekuwa na tafiti nyingi sisi unaweza ukatoa motisha tena kubwa kabisa lakini mwisho wa siku matokeo yakawa ni yale yale tunashauri unapo muahidi aonyeshe mabadiliko ndio umpe motisha sio malipo tuite bakishishi kinacho mpoza baada ya matokeo kuwepo.”

Ikumbukwe rasimu mpya ya Sera ya Elimu na Mafunzo, iliwasilishwa bungeni Dodoma katika bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia Mei 16, 2023 ambapo wizara inaendelea kupokea maoni kuhusu sera hiyo hadi Mei 31, 2023 na Juni mwaka huu wizara inatarajiwa kuomba idhini ili kuwezesha utekelezaji wake.

Imetayarishwa na mwandishi wetu Amri Ramadhani, Sauti ya Amerika, Tanzania

XS
SM
MD
LG