Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 15:49

Tanzania yasimamisha usajili wa meli za Kimataifa


Serikali ya Tanzania imesimamisha kwa muda usajili wa meli za mataifa mengine baada ya matukio ya hivi karibuni ya kukamatwa kwa meli tano zinazopeperusha bendera ya Tanzania zikiwa zimebeba bidhaa haramu.

Rais John Magufuli Ijumaa aliamrisha pia mamlaka za nchi hiyo kufanya uchunguzi wa kina katika usajili wa meli 470 ambazo hivi sasa zinasafiri katika bahari za kimataifa zikiwa na bendera ya Tanzania.

Mapema Januari serikali ya Ugiriki ilikamata meli yenye bendera ya Tanzania karibu na kisiwa cha Crete ikiwa njiani kuelekea Libya huku ikiwa imebeba vilipuzi. Libya imekuwa chini ya vikwazo vya silaha ilivyowekewa na Umoja wa Mataifa mwaka 2011

Wiki chache kabla ya hapo, meli nyingine yenye bendera ya Tanzania ilikamatwa katika bahari ya Atlantic ikiwa imebeba tani 1.6 za madawa ya kulevya.

Tanzania pia ni moja ya nchi saba ambazo zinachunguzwa na Umoja wa Mataifa kwa kukiuka marufuku ya silaha dhidi ya Korea Kaskazini. Marekani imekuwa ikiweka shinikizo kwa Tanzania na nchi nyingine nne za Afrika ziwache kuruhusu meli za Korea Kaskazini kutumia bendera zao.

Vyanzo vya habari Tanzania vinasema meli hizo za nchi za nje mara kwa mara zinasajiliwa na kampuni ya usajili wa meli za kimataifa iliyopo katika kisiwa Zanzibar.

XS
SM
MD
LG