Sudan Kusini imemuita nyumbani balozi wake anayeiwakilisha nchi hiyo nchini Marekani baada ya utawala wa Rais Trump kuweka vikwazo vya silaha kwa serikali ya Sudan Kusini wiki iliyopita.
Makamu Rais wa kwanza wa Sudan Kusini, Taban Deng Gai alisema hatua hiyo ya Marekani itadumaza juhudi za kutatua kwa amani ugomvi uliyopo nchini mwake. “Balozi Garang Diing ameitwa kurudi Juba. Wanafahamu inamaana kidiplomasia” alisema Gai wakati akifunga sherehe za maadhimisho ya siku ya umoja wa kitaifa Sudan Kusini kwenye uwanja wa kitaifa mjini Juba.
Gai alisema vikwazo vya silaha vilivyowekwa na Marekani vimekuja kwa kushtukiza wakati ujumbe wa serikali ya Sudan Kusini ulijiandaa kuelekea Addis Ababa nchini Ethiopia kuhudhuria awamu ya pili ya mkutano wa ngazi ya juu wa kurejesha amani ambao ulilenga kufufua mkataba wa amani wa mwaka 2015.
Vyama hasimu huko Sudan Kusini vilitia saini mkataba wa kusitisha mapigano mwishoni mwa mkutano wa awamu ya kwanza mwezi Disemba, utaratibu ambao ulikiukwa na pande zote mbili ndani ya muda wa siku kadhaa.