Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 06:01

Vyama vya kisiasa Somalia vyatia saini makubaliano


Rais wa Somalia Sheikh Sharif Sheikh Ahmed (kati) akipeana mkono na mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kwa Somalia, Augustine P.Mahiga
Rais wa Somalia Sheikh Sharif Sheikh Ahmed (kati) akipeana mkono na mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kwa Somalia, Augustine P.Mahiga

Mazungumzo ya kuleta amani nchini Somalia yamemalizika na kutoa makubaliano kwa pande zote kujituma na kujitolea kuijenga upya nchi ya Somalia

Makundi makuu ya kisiasa nchini Somalia yalimaliza mazungumzo yao ya siku tatu mjini Addis Ababa Ethiopia Jumatano kwa kusema kuwa yamejitolea kuona mchakato wa amani wa mabadiliko ya kiutawala nchini mwao ifikapo mwezi Agosti mwaka huu.

Washiriki wa mkutano huo uliodhaminiwa na Umoja wa Mataifa walionyesha muungano usio wa kawaida huku kukiwa na masuala tete ya kujadiliwa ambayo kwa kawaida huwa magumu kuyajadili baina ya koo mbalimbali zinazozozana huko Somalia. Mwishowe vyama vyote sita vilikubaliana kuweka kando masuala mengi mazito pamoja na yale madogo madogo kwa maslahi ya kuwa na serikali thabiti baada ya siku 90 ambapo utawala wa serikali ya mpito ndipo utakapofunga shughuli zake.

Waziri mkuu wa serikali ya mpito Abdiweli Mohammed Ali ambaye anaonekana kuongoza juhudi za kile kinachoitwa mkakati mpya wa ratiba kuelekea utawala mpya alisema motisha kwake inatokana na mapenzi ya kuona mzozo wa Somalia umeisha na taifa hilo limeondolewa kwenye orodha ya nchi zilizoshindwa kabisa kuwa na uthabiti wa kisiasa.Makubaliano yaliyotiwa saini Addis Ababa Jumatano baada ya mazungumzo kumalizika yanazitaka pande zote husika kujituma na kujitolea kuijenga upya Somalia.

Makubaliano hayo pia yanatoa mwito kuwe na bunge katika muda wa mwezi mmoja na katiba ya muda ifikapo Julai 10 ambayo itafuatiwa na kuapishwa kwa wabunge siku 10 baadaye na kukamilisha kipindi cha serikali ya mpito kabla ya tarehe ya mwisho ya Agosti 20 ambapo serikali ya mpito inatakiwa kumaliza ramsi shughuli zake.

Rais wa serikali ya mpito Sheikh Sharif Sheikh Ahmed ambaye huenda akapoteza wadhifa wake huo baada ya hatua hizo kutekelezwa alisifu mwamko mpya wa umoja na ushirikiano miongoni mwa makundi mbalimbali na koo ambazo kihistoria zimekuwa zikizozana nchini Somalia.

XS
SM
MD
LG