Hatua hiyo ni kufuatia kilio cha umma kutokana na ongezeko kubwa la ubakaji wa wasichana na wanawake nchini humo. Serikali itahitajika kubuni mahakama maalum kote nchini ili kuharakisha kesi dhidi ya washukiwa wa ubakaji, ikiwezekana ndani ya miezi minne.
Sheria hizo pia zimetoa idhini ya kuwepo kwa orodha ya kitaifa ya washukiwa wote wa dhuluma za kingono kwa msaada wa idara ya kitaifa ya kukusanya data. Taarifa kuhusu waathirika zitakuwa siri wakati kukiwa na vyumba maalum vya kuwapatia ushauri pamoja na kuwapa huduma za kiafya muda mfupi baada ya ubakaji kutokea. Watakaopatikana na hatia ya ubakaji wa kundi watahukumiwa kifo au kifungo cha maisha.
Wale watakaopatikana na hatia ya kurudia watahasiwa kwa kutumia kemikali. Wakosoaji wanasema kwamba ni chini ya asilimia 4 ya kesi za ubakaji nchini Pakistan, ambazo hutolewa hukumu. Hata hivyo wanaharakati wa haki za binadamu wamekaribisha hatua hiyo wakisema kwamba kunahitajika uimarishaji wa sera pamoja na idara ya kuongoza mashitaka ili kuhakikisha haki inapatikana.