Mahakama Kuu ya Kenya Alhamisi iliamuru serikali ilipe fidia kwa wanawake wanne walioathiriwa na wimbi la unyanyasaji wa kijinsia ambalo liliibuka katika ghasia za baada ya uchaguzi uliopingwa wa mwaka 2007.
Wote wanne watapokea sawa na karibu dola 36,000, wakati walalamikaji wengine wanne wanawake wawili na wanaume wawili kesi zao zilitupwa nje.
Mahakama kuu ilisema Serikali inawajibika kwa kushindwa kufanya uchunguzi huru na ulio bora wa mashtaka ya uhalifu wa unyanyasaji wa kingono na kijinsia wakati wa ghasia za baada ya uchaguzi. Matokeo yake, ilisema ilikuwa ni ukiukaji wa haki zao za kikatiba.
Ni uamuzi wa kihistoria: Madaktari wa taasisi ya haki za binadamu
Madaktari wa Haki za Binadamu taasisi ya hisani ambayo ilisaidia kupeleka kesi hiyo kortini, ilipokea vyema uamuzi huo wa kihistoria, wakisema ni mara ya kwanza nchini Kenya kwamba unyanyasaji wa kijinsia baada ya uchaguzi umetambuliwa na serikali, na fidia kutolewa.
Naitore Nyamu, Mkuu, wa madaktari wa Haki za Binadamu (PHR) Kenya anasema kwamba uamuzi wa kihistoria umetolewa na mahakama kuu ya Kenya.
"Baada ya miaka saba ya kungoja na kucheleweshwa, leo waathirika wa unyanyasaji wa kijinsia wanaweza kupata pumziko la furaha kwa sababu leo mahakama kuu imetoa haki kwa waathirika wa unyanyasaji wa kijinsia. Huu ni uamuzi mzuri ambao hautakuwa na athari tu nchini Kenya, lakini ulimwenguni kote kutokana na masuala ya ulinzi, uchunguzi, na mashtaka ya kesi za unyanyasaji wa kijinsia na kingono” alisema Nyamu.
Miezi kadhaa ya vurugu iligubika Kenya kufuatia uchaguzi wa urais uliopingwa mnamo mwaka 2007. Vikundi vya haki viligundua kuwa zaidi ya watu 1,100 waliuwawa na watu wasiopungua 900 walinyanyaswa kingono, pamoja na ubakaji wa genge na kuhasiwa.
Miaka kadhaa baadaye, Mahakama ya Kimataifa ya Jinai -ICC huko The Hague iliwafungulia mashtaka Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta na naibu wake William Ruto kwa uhalifu dhidi ya binadamu, lakini kesi zote mbili zilishindikana baada ya mashahidi kushindwa kutoa ushahidi wao. Katika uamuzi wake Alhamisi mahakama pia ililipa gharama.
“Gharama za uharibifu huu zimetolewa kwa waathirika wanne tu kati ya wanane waliowasilisha malalamiko na hawa wanne ni wanawake ambao wamelipwa Shilingi milioni nne za Kenya (karibu dola $ 36,000) kila mmoja wao” aliongeza Nyamu.
Mmoja wa waathirika aliyelipwa fidia alisema, "Tunayo furaha kuwa korti hatimaye imetambua madhara ambayo tulipata . Walakini, hatuelewi ni kwanini korti ilitutenga na haikutoa fidia kwa waathirika wengine wanne. Lakini Nyamu aliongeza kuwa uamuzi huo ulikuja kwa wakati muafaka.
Vurugu pamoja na unyanyasaji wa kingono inaendelea kuwa mada kuu katika uchaguzi wa urais nchini Kenya, ambapo uchaguzi unaofuata utafanyika ifikapo Agosti 2022.
Imetayarishwa na Sunday Shomari, VOA, Washington DC