Rais wa Sudan Kusini, Salva Kiir, ametangaza serikali mpya ya Umoja wa Kitaifa na kuwaleta pamoja wanasiasa kutoka upande wa upinzani waliokuwa katika vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini humo.
Rais Kiir aliwataja mawaziri 30, 14 kati yao walichaguliwa na kiongozi wa waasi ambaye sasa ni Makamu Rais Riek Machar na makundi mengine ya kisiasa. Mawaziri hao waliapishwa leo Ijumaa kwenye sherehe zilizofanyika katika mji mkuu Juba.
Kuundwa kwa serikali mpya ni hatua muhimu sana kuelekea katika utekelezaji wa mkataba wa Amani uliotiwa saini na Kiir na Machar, mwezi Agosti mwaka jana.
Mkataba huo wa Amani unatoa wito kwa serikali ya mpito kutekeleza mageuzi ya kiuchumi na kijeshi, kuielekeza nchi kwenye uchaguzi ndani ya kipindi cha miezi 30 na kushirikiana na mahakama ambayo itawahukumu washutumiwa waliohusika na vitendo vya ukatili wakati wa vita.