Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 08:57

Saudi Arabia yaijulisha Marekani hujuma iliyopangwa na Iran


Rais wa Marekani Joe Biden akisalimiana na Mwana wa Mfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman
Rais wa Marekani Joe Biden akisalimiana na Mwana wa Mfalme wa Saudi Arabia Mohammed bin Salman

Saudi Arabia imeshirikiana na maafisa wa Marekani taarifa za kijasusi zinazoonyesha Iran huenda ikawa inajiandaa kwa shambulizi dhidi ya ufalme huo, maafisa watatu wa Marekani wamesema siku ya Jumanne.

Ongezeko la wasiwasi huo kuhusu uwezekano wa shambulizi dhidi ya Saudi Arabia umekuja wakati uongozi wa Biden unaikosoa Tehran kutokana na kuwakamata waandamanaji nchi nzima na kulaani kitendo chake cha kupeleka mamia ya droni – na msaada wa kiufundi -- Russia ili wazitumie katika vita vyake na Ukraine.

“Tuna wasiwasi kuhusu tishio hili, tunaendelea kuwa na mawasiliano ya mara kwa mara ya kijeshi na kijasusi na Wasaudi,” Baraza la Usalama la Taifa limesema katika taarifa yake. “Hatutasita kuchukua hatua kulinda maslahi yetu na washirika wetu katika eneo hilo.”

Saudi Arabia haikujibu ilipotakiwa kutoa maoni yake. Ubalozi wa Iran huko Umoja wa Mataifa umeliambia shirika la habari la AP Jumatano kuwa madai ya Marekani “hayana msingi.”

“Tawala wa Magharibi na Wazayuni zinasambaza habari za upande mmoja kwa lengo la kutengeneza hisia mbaya dhidi ya Jamhuri ya Kiislam ya Iran na kupotosha mwelekeo mzuri ulioko hivi sasa na nchi za eneo,” ubalozi huo ulieleza katika taarifa yake.

Mmoja wa maafisa aliyethibitisha ripoti hiyo ya kijasusi alieleza tishio hilo ni la uhakika la kufanyika shambulizi “karibuni au katika saa 48.”

Hakuna ubalozi wa Marekani au ubalozi mdogo katika eneo uliotoa tahadhari au muongozo kwa Wamarekani wanaoishi Saudi Arabia au sehemu nyingineza Mashariki ya Kati kuhusu habari hizo za kijasusi.

Maafisa hao hawakuidhinishwa kutoa maoni yao kwa umma, wamezungumza kwa sharti la kutotajwa majina yao.

Alipoulizwa kuhusu ripoti hizo za kijasusi walizoshirikiana na Wasaudi, Brigadia Jenerali Pat Ryder, msemaji wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani, alisema maafisa wa jeshi la Marekani “wana wasiwasi kuhusu tishio hilo katika eneo hilo.”

“Tunafanya maasiliano ya mara kwa mara na washirika wetu Saudi Arabia, katika misingi ya habari gani wanaweza kuwa nazo ili watupatie kutoka eneo lao,” Ryder alisema.

“Lakini tulichosema hapo kabla, nitarejea kusema, ni kuwa tutashikilia haki ya kujihami na kujilinda wenyewe bila ya kujali wapi majeshi yetu yanatumika, iwe in Iraq au kwingineko.”

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje Ned Price alisema Marekani ina “wasiwasi kuhusu tishio hilo,” bila ya kufafanua.

Jarida la The Wall Street mara ya kwanza liliripoti juu ya Saudia kushirikiana habari hizo za kijasusi mapema Jumanne. Iran imedai bila ya kutoa ushahidi kwamba Saudi Arabia na mahasimu wao wengine wanawachochea raia wa kawaida kufanya uasi katika mitaa ya Iran.

Chanzo cha habari hii ni shirika la habari la AP

XS
SM
MD
LG