Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 09:20

Russia yashambulia Lviv na Kyiv ikitishia kutumia makombora ya masafa marefu


Mwanajeshi wa Ukraine akitumia silaha wakati wa mazoezi ya kijeshi huko mkoa wa Lviv.
Mwanajeshi wa Ukraine akitumia silaha wakati wa mazoezi ya kijeshi huko mkoa wa Lviv.

Ndege za kivita za Russia zimeshambulia kwa mabomu mji wa Lviv na kwa makombora mji mkuu wa Kyiv Jumamosi, na kusababisha kifo cha mtu mmoja baada ya karibu wiki mbili za utulivu katika mji mkuu wa Ukraine.

Kuongezeka kwa mashambulizi kunatokea siku moja baada ya Moscow kutoa tena vitisho vya kushambulia kwa makombora ya masafa marefu miji mbalimbali ya Ukraine baada ya manwari yake kuu ya kivita Moskova kuzama katika bahari ya Black Sea.

Mashambulio makali yanaripotiwa pia upande wa mashariki wa Ukraine ambako kombora moja limeshambulia kiwanda cha kusafisha mafuta ya petroli katika mji wa Lyssytchansk.

Moscow imesema ndege zake zimeshambulia kiwanda cha kukarabati vifaru katika mji mkuu, ambako mlipuko ulisikika na moshi ulionekana katika wilaya ya Darnystskyi iliyoko kusini mashariki. Meya wake alisema waokoaji na madaktari walikuwa wako kazini huko lakini hakutoa ufafanuzi zaidi.

Manuari ya kivita Moskva ya Russia
Manuari ya kivita Moskva ya Russia

Jeshi la Ukraine lilisema ndege za kivita za Russia zilizokuwa zimeruka kutoka Belarus zilipiga makombora katika mkoa wa Lviv karibu na mpaka wa Poland, ambako makombora yalitunguliwa na ulinzi wa anga wa Ukraine.

Waandishi wa habari wa Reuters wamefika katika mji wa Ilyich ulokua unashikiliwa na Russia ambako kunapatikana kiwanda kikubwa cha chuma, ambacho Moscow ilikuwa imedai imekikamata Ijumaa, moja ya viwanda viwili vikubwa vya chuma ambako walinzi wamejificha katika madaraja na mahandaki ya chini ya ardhi.

Kiwanda hicho kimeharibiwa na kuwa ni ghofu lenye vyuma vilivyopinda na zege lililopasuka, na hakuna alama ya waliokuwa wanalinda kuwepo.

Nje, kiasi cha nusu darzeni ya miili ya raia ilikuwa imetawanyika katika mitaa ya karibu, ikiwemo mwanamke mwenye nguo ya pinki na viatu vyeupe.

Kuna mtu alikuwa amechora kwa rangi “neno mined” katika ukuta upande wa uwanja wa mbele wa kituo cha mafuta kilichokuwa kimeharibiwa. Ikiwa ni nadra kuona alama ya uhai, gari moja jekundu lilikuwa inapita polepole katika mtaa uliokuwa mtupu, neno “watoto” lilikuwa limeandikwa katika kadi iliyokuwa imebandikwa kwa gundi kwenye kioo cha mbele cha gari.

Jengo la serikali likiwaka moto huko Mykolaiv, Ukraine kufuatia shambulizi la Russia , Jumatano March 30, 2022. Raia 15 waliuawa katika shambulizi hilo. (AP Photo/Petros Giannakouris)
Jengo la serikali likiwaka moto huko Mykolaiv, Ukraine kufuatia shambulizi la Russia , Jumatano March 30, 2022. Raia 15 waliuawa katika shambulizi hilo. (AP Photo/Petros Giannakouris)

Huko Mykolaiv, mji mwingine ulioko karibu na mstari wa mbele huko kusini, Russia imesema ilikuwa imekishambulia kiwanda cha kukarabati magari ya kijeshi.

Mashambulizi ya mabomu na makombora yamefuatia tangazo la Russia Ijumaa kuwa itaendeleza zaidi mashambulizi ya masafa marefu kwa kulipiza kisasi dhidi vitendo vya “hujuma” na “ugaidi” ambavyo havijafafanuliwa saa kadhaa baada ya kuthibitisha kuzama kwa meli yake ya kitaifa Moskva katika bahari ya Black Sea.

Kyiv na Washington wanasema meli hiyo ilipigwa na makombora ya Ukraine, shambulizi linaloonyesha mafanikio ya Jeshi la Ukraine dhidi ya adui mwenye silaha bora zaidi. Moscow inasema meli hiyo ilizama baada ya kushika moto.

Mwezi mmoja na nusu wa uvamizi unaofanywa na Rais Vladimir Putin huko Ukraine, Russia inajaribu kukamata eneo upande wa kusini na mashariki baada ya kujiondoa upande wa kaskazini kufuatia mashambulizi makubwa dhidi ya Kyiv yaliyozimwa katika maeneo nje ya mji mkuu.

Majeshi ya Russia yalijiondoa kutoka kaskazini wakiiacha miji ikiwa na miili ya raia iliyotawanyika, ushahidi wa kile Rais wa Marekani Joe Biden wiki hii alikiita mauaji ya kimbari – jaribio la kutaka kufuta kabisa utaifa wa Waukraine.

Russia imekanusha kulenga raia na inasema lengo ya kile inachokiita ni “operesheni maalum ya kijeshi” ni kuwanyang’anya silaha, kuwashinda wazalendo na kuwahami waliowachache katika eneo la kusini mashariki.

XS
SM
MD
LG