Kiongozi wa uasi Sudan Kusini ambaye ni makamu wa rais wa kwanza mteule Riek Machar anatarajiwa kurejea mjini Juba Jumanne.
Waziri wa habari wa Sudan Kusini, Michael Makuei, amesema kurejea kwa Machar ni hatua kubwa katika kutekeleza makubaliano ya Amani yaliyofanyika mwaka jana kati yake na Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini.
Machar alitarajiwa kufika Juba mapema Jumatatu lakini msemaji wa kundi la waasi amesema kuwa amechelewa kutokana na ndege kushindwa kupata kibali cha kuruka na hivyo kuwepo uchelewesho hadi Jumanne asubuhi.
Waziri Makuei amesema kuwa Machar ataapishwa kuwa makamu rais wa kwanza pindi tu atakapowasili Juba ikiashiria mwanzo wa miezi 30 ya kipindi cha mpito.
James Wani Igga makamu rais wa sasa atakuwa makamu wa pili wa rais baada ya Machar kuapishwa kushika madaraka katika serikali mpya.