Rais wa Brazil Luiz Inacio Lula da Silva, amemfukuza kazi afisa wa ngazi ya juu katika idara ya ujasusi nchini humo kufuatia uchunguzi wa tuhuma za ujasusi kinyume cha sharia, unaomhusisha mtoto wa rais wa zamani Jair Bolsonaro.
Kufukuzwa kazi kwa Alessandro Moretti, kama mkurugenzi msaidizi wa shirika hilo, linalojulikana kwa kifupi ABIN kumekuja siku moja baada ya polisi kuvamia nyumba inayohusishwa na Carlos Bolsonaro, diwani wa jiji la Rio de Janeiro.
Jaji wa Mahakama Kuu Alexandre de Moraes, alitoa waranti kwa ajili ya uvamizi kwenye nyumba na ofisi ya Carlos Bolsonaro kwa msingi wa madai ya polisi wa serikali kuu, juu ya kuwepo kwa kikundi ndani ya ABIN ambacho kiliwashambulia wapinzani wa Jair Bolsonaro wakati wa kipindi cha urais wake wa miaka minne, ambao ulimalizika mwaka 2022.
Wachunguzi wanashuku Alexandre Ramagem, ambaye aliendesha ABIN chini ya Bolsonaro, alitumia programu inayojulikana kama FirstMile iliyotengenezwa na kampuni ya Israeli, kufuatilia wanasiasa na watu maarufu. Polisi walivamia ofisi ya Ramagem na nyumbani kwake wiki iliyopita.
Forum