Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Septemba 29, 2023 Local time: 09:39

Maelfu ya Wasomali Waandamana Kumuunga Mkono Rais Mohamed Abdullahi Farmajo


Rais Mohamed Abdullahi Farmaajo

Maelefu ya watu wameingia mitaani katika miji mikubwa ya Somalia Alhamisi, wakisherehekea ushindi wa rais mteule wa nchi hiyo, Mohamed Abdullahi Farmajo.

Mjini Mogadishu, mji mkuu wa Somalia, makundi ya wananchi walikuwa wakishangilia na kuimba wimbo ya taifa huku wakiandamana katika mitaa Alhamisi asubuhi, hukui vikosi vya usalama vikirusha risasi hewani, kama ishara ya furaha yao.

Sherehe kama hizo pia zimefanyika katika miji mikubwa mingine nchini Somalia, ikiwemo Beledweyne, Jowhar, Garbarey, Abudwaq na Kismayo na maeneo mengine.

Amani ndio matumaini yao

Wengi waliokuwa wakisherehekea ushindi huo walikuwa wakitaja amani, utulivu na serikali kuwajibika kuwa ndio vitu muhimu kwao.

“Siku zote nimekuwa nikifikiria kwamba siku moja Somalia itasimama yenyewe, na Mogadishu itakuwa ndio makao yake makuu, itarudisha sura yake nzuri mara nyingine,” amesema Liban Ahmed, mkazi wa Mogadishu.

“Mimi ni mkazi wa kudumu Mogadishu na nimeweza kushuhudia mabaya yote na mazuri. Lakini kitu kimoja nina hakika nacho ni kuwa sijakata tamaa.”

Mkazi mwingine, Omar Aden, 45, mwenye kumiliki mgahawa, baba wa watoto 10 amesema, “Kila uchaguzi wa Somalia baada ya 1991 uliamsha matumaini yake kuwa hali itakuwa bora zaidi.

“Sisi tumeshuhudia chaguzi mbalimbali na nyakati tofauti zenye hali ngumu, lakini siku zote nimechukulia zoezi la demokrasia kama ni dalili njema ya kurejea kwa amani na utaifa wa Somalia,” Aden amesema.

Historia ya Chaguzi za Somalia

Lakini anasema matumaini ya kuwa na rais mtekelezaji na mwenye uongozi bora ulifikia kileleni mnamo Septemba 2012 wakati Somalia ilipochagua serikali yake katika miongo miwili.

Watu walidhania kuwa miaka mingi ya mapigano, machafuko, ugaidi na uharamia ilikuwa inafikia kikomo, hisia za ndani ambazo hazijaondoka kutoka katika ndoto za Wasomali wa kawaida.

Lakini uongozi unaoondoka madarakani wa Rais Hassan Sheikh Mohamud umeshindwa kukidhi matarajio ya umma.

Hali ya usalama ni tata, na nchi hiyo ni namba moja katika orodha ya mataifa yaliyokumbwa na ufisadi.

Matokeo ya Uchaguzi

Mohamed, ambaye ana umri wa miaka 55, alitangazwa na bunge la Somalia Jumatano kuwa mshindi baada ya raundi ya pili ya upigaji kura, kufuatia mchakato wa uchaguzi kucheleweshwa mara kadhaa zilizopelekea kuundwa kwa bunge lilioko hivi sasa.

Mara tu alipoapishwa baada ya kupigiwa kura kwenye ukumbi ambao ulikuwa umezungukwa na kuta zenye uwezo wa kuzuia milipuko ya mabomu katika uwanja wa ndege wa mji mkuu huo.

Uchaguzi wake umewapa mamilioni ya wananchi matumaini katika nchi maskini na iliyokumbwa na machafuko ambayo hivi sasa inakabiliana na hali mbaya sana ya ukame.

Akilihutubia taifa kupitia vyombo vya habari vya serikali Jumatano usiku, rais mteule mpya Mohamed Abdullahi Farmajo amesema ilivyokuwa kwamba amechaguliwa kwa matakwa ya watu wa Somalia, anapanga kuunda serikali itakayo jikita katika ushirikiano wa umma.

“Mpango wangu ni kuunda serikali inayo waunganisha watu wa kawaida na viongozi wao. Serikali ya kiraia ambayo inafanya kazi kwa kushirikiana na wananchi wake pande zote zikiwemo za usalama na uchumi,” rais amesema.

Matumaini makubwa

Mohamed ameonekana kuwa moja wa wanasiasa maarufu sana katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika ambaye hajawahi kuonekana baada ya kuanguka utawala mkuu wa serikali ya nchi hiyo mwaka 1991.

Katika kipindi kifupi alichotumikia kama waziri mkuu- tangu 2010 mpaka 2011- alipata sifa kwa kuwa mchapakazi na mwenye uzalendo.

Dr Abdinur Sheikh ambaye aliwahi kuwa waziri wa elimu katika baraza la mawaziri la Mohamed amesema alipata sifa kwa kuunda baraza la mawaziri lenye mawaziri wachache na kuchagua wataalamu.

“Wengi walisifia baraza lake hilo ambalo mimi nilikuwa moja ya wateule wake kwa kuwa baraza la mawaziri lilikuwa na wasomi zaidi na wataalamu kutoka Marekani na Ulaya,” Abdinur amesema.

Mohamed aliacha kazi hiyo wakati wa mvutano wa uongozi kati ya aliyekuwa rais na spika wa bunge, kitendo kilichopelekea wananchi wa Mogadishu kuandamana mitaani, wakimtaka abakie madarakani.

Kampeni za Urais

Katika kampeni yake ya urais, alitoa ahadi kwamba atapiga vita ufisadi katika taifa hilo ambalo linategemea misaada na kuwa kipato cha nchi hiyo kidogo kinachotokana na kodi zinazokusanywa uwanja wa ndege wa Mogadishu na bandarini hazitatumika vibaya au kutumika kwa ajili ya safari za nje.

Aliungwa mkono kwa nguvu na wafanyakazi wa vyombo vya usalama vya nchi hiyo kutokana na kuhimiza kwake juu ya kulipwa kwa wakati jeshi la polisi, usalama and majeshi ya ulinzi ya Somalia ambao wanapambana na kikundi cha wapiganaji wa al-Shabab

Mwaka 2011 Mohamed aliamuru mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayoshugulikia Somalia, lakini yalikuwa na makao yake katika nchi jirani ya Kenya wakati huo kwa sababu za kiusalama, kuhamia Mogadishu akiwapa miezi mitatu, uamuzi mgumu ambao Wasomali wengi waliufurahia.

Mohamed alielezea katika agizo lake hilo kwa UM kwamba ofisi kama hizo mbona ziko katika nchi nyingine zenye matatizo kama vile Iraq na Afghanistan.

Wasemavyo Wachambuzi

Husein Abdikarim Ginidish ni mchambuzi wa masuala ya kisiasa Somalia anayeishi North Carolina ambaye anamjua Mohamed amesema Wasomali wanampenda kwa sababu yeye ni mwanasiasa ambaye ni muwazi kwa wanaomkosoa na kumpa maoni yenye manufaa.

“Ni mwanasiasa mpole, mnyenyekevu na mtendaji. Na kwa kweli ni mtu ambaye anasikiliza ushauri wa pande zote; wanaompinga na marafiki zake. Nafikiri ndilo lililomfanya awe maarufu kwa watu wa kawaida,” amesema Gindish.

Wasomali wengi ulimwenguni, ambao walikuwa na wasiwasi uchaguzi wa rais utafuata njia ile ile ya ufisadi katika mchakato wa uchaguzi ambao ndio ulioweka madarakani Bunge la sasa, na sasa limebadilika kuwa ni harakati za kupinga ufisadi.

Wengine wanafikiria kuwa ilikuwa ni hatua kubwa katika kuijenga tena Somalia- ikiwa tu kuna zoezi la kufananisha juhudi hizo na demokrasia.

XS
SM
MD
LG