Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 08:26

Raia wa Kenya ashikiliwa na mamlaka za DRC kufuatia shambulizi lililouwa watu 10


Mmoja wa majeruhi wa shambulizi la kigaidi lililotokea katika kanisa moja mjini Kasindi, wilaya ya Beni, DRC.
Mmoja wa majeruhi wa shambulizi la kigaidi lililotokea katika kanisa moja mjini Kasindi, wilaya ya Beni, DRC.

Mamlaka  nchini Kongo  inamshikilia  raia mmoja wa Kenya anayeshukiwa kuwa mwanachama  katika kundi la kigaidi  lililopigwa marufuku nchini Uganda, Allied Democratic Forces (ADF).

Mtu huyo inasemekana alipanga shambulizi la Jumapili kwenye kanisa lililoko Kivu Kaskazini ambapo watu 10 waliuwawa.

Mamlaka nchini Kongo haijatoa jina la mshukiwa huyo wakati alipokamatwa Jumapili, lakini kitengo cha polisi Kenya kinachopambana na ugaidi (ATPU) Jumatatu kimemtaja mtuhumiwa kuwa ni Abdirizak Muktar Garad, mwenye umri wa miaka 29, mkazi kutoka kaunti ya Wajir , kaskazini mwa Kenya.

Mmoja wa majeruhi wa shambulizi la kigaidi lililotokea katika kanisa moja mjini Kasindi, wilaya ya Beni, DRC.
Mmoja wa majeruhi wa shambulizi la kigaidi lililotokea katika kanisa moja mjini Kasindi, wilaya ya Beni, DRC.

Tukio la Kasindi, Kivu Kaskazini, karibu na mpaka wa Uganda limewaacha takriban watu 39 wakiwa wamejeruhiwa, kwa mujibu wa idadi ya awali iliyotolewa na jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (FARDC).

Msemaji wa FARDC katika eneo hilo Anthony Mualushayi amesema Jumapili, kuwa , baada ya uchunguzi wa awali kwenye eneo la tukio la janga hilo, raia wa Kenya alikamatwa kwa kuwa na mahusiano katika kupanga shambulizi ambalo sasa linahusishwa na ADF.

Maafisa wa Jeshi la DRC wakiwa katika eneo la tukio la shambulizi.
Maafisa wa Jeshi la DRC wakiwa katika eneo la tukio la shambulizi.

Mpaka hivi sasa hakuna kundi lolote la kigaidi lililodai kuhusika na shambulizi hilo, lakini jeshi la Kongo limelihusisha na kundi la ADF, kundi hilo la kigaidi la Uganda lina makao yake mwa Kongo, ambapo katika siku za nyuma lilishambulia vijiji nchini DRC na kuanzisha mashambulizi katika maeneo ya mjini nchini Uganda.

Magaidi wa ADF, wengi wao wanaaminika kutokea nchini Uganda, na hufanyia operesheni zao huko Kivu Kaskazini na Ituri mashariki mwa DRC.

Chanzo cha habari hii ni gazeti la "The East African" linalochapishwa nchini Kenya.

XS
SM
MD
LG