Polisi nchini Msumbiji wamewekwa katika hali ya tahadhari, wakijitayarisha kwa maandamano zaidi ya kupinga ongezeko la bei ya chakula nchini humo.
Siku tatu za maandamano na machafuko wiki iliyopita zilisababisha vifo vya watu 10 na wengine zaidi ya 400 kujeruhiwa. Polisi wanasema ujumbe wa simu usiojulikana chanzo unasambazwa nchini, ukihimiza watu kuanza tena maandamano Jumatatu.
Mji mkuu, Maputo, ulikuwa shwari Jumapili, lakini polisi wanasema wanafanya doria katika mitaa kuzuia marudio ya machafuko.
Maandamano yalianza Maputo Jumatano baada ya serikali kutangaza ongezeko la bei ya chakula kama vile mkate, maji na umeme.