Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Aprili 25, 2024 Local time: 01:38

Papa Francis afananisha manyanyaso ya ngono kwa watoto na kafara za kipagani


Waathirika wa manyanyaso ya ngono wakilaani vitendo waliofanyiwa na viongozi wa kanisa mbele ya eneo la Mtakatifu Peter Square, Vatican, Feb. 24, 2019.
Waathirika wa manyanyaso ya ngono wakilaani vitendo waliofanyiwa na viongozi wa kanisa mbele ya eneo la Mtakatifu Peter Square, Vatican, Feb. 24, 2019.

Kiongozi wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis ameahidi hatua thabiti zitachukuliwa kupambana na manyanyaso ya ngono wanaofanyiwa watoto wakati mkutano wa Kanisa Katoliki ukimalizika uliyozungumzia watu wanaowaharibu watoto wadogo.

Viongozi wa dini ambao wanawaharibu watoto ni “zana za shetani,” Papa amesema, akiahidi kukabiliana na kila tukio la aina hiyo “kwa kuchukuwa hatua kali kabisa,” Shirika la habari la Uingereza BBC limeripoti Jumapili.

Historia ya unyanyasaji wa watoto

Vitendo vya kuwaharibu watoto, amesema, vinamkumbusha vitendo vya dini za kale ambapo watoto walikuwa wanatolewa muhanga katika maeneo ya ibada ya wapagani.

Azimio la mkutano huu wa kupambana na vitendo vya manyanyaso ya ngono kwa watoto duniani, kuanzia sasa viongozi wa dini watatakiwa kupitia upya na kuboresha miongozo yao ili kuepusha unyanyasaji huo na kuwaadhibu wale wote wanaoendeleza vitendo hivyo, ameongeza.

Papa amezungumza kwa kutumia kauli ya hali ilivyo kwa ujumla, lakini waathirika na walionyanyaswa ambao wanaendelea kuishi watataka maelezo ya hatua zinazoweza kuchukuliwa na kanisa zitangazwe wazi, amesema mwandishi wa habari wa BBC huko Vatican, James Reynolds.

Kanisa linawajibu wa kusimamia maadili, ukweli

“Jambo hili linanikumbusha vitendo vya kikatili vya kidini, ambavyo vilikuwa vimeenea katika baadhi ya tamaduni za kuwatoa muhanga binadamu – mara nyingi watoto – katika maeneo ya ibada ya wapagani,” amesema Papa wakati wa kufunga mkutano wa siku nne uliofanyika Vatican.

“Kukosekana ubinadamu katika matukio mbalimbali kama haya ulimwenguni inafanya jambo hilo kuwa baya zaidi na kashfa zaidi katika Kanisa hili, kwa sababu inakinzana na jukumu la kusimamia maadili na miongozo ya haki.

“Mtu mtakatifu, ambaye amechaguliwa na Mungu kuongoza roho kufikia uokovu, anakubali udhaifu wake wa kibinadamu umtawale, au maradhi yake mwenye yamtawale na hivyo kuwa chombo cha Shetani. Katika manyanyaso ya ngono tunaona mkono wa shetani ambao haumuachi hata mtoto asiye na hatia," amefafanua Papa Francis.

Kanisa kuchukuwa hatua za kisheria

Papa amesema kuwa walioathirika hivi sasa watakuwa ndio kipaumbele na kuahidi kumalizika kwa vitendo vya kuwaficha waliohusika, akisema wote walioshiriki katika unyanyasaji huo sheria itachukuwa mkondo wake.

Pia amesisitiza kuwa manyanyaso ya ngono kwa watoto ni tatizo lilioko duniani kote – “ni matendo yaliyoenea katika tamaduni zote na jamii zote”.

Mkutano huo ambao ni wa aina yake ambao haujawahi kufanyika miaka ya nyuma – ulitoa wito watoto wote walindwe Makanisani – ulihudhuriwa na viongozi wa Kanisa Katoliki wa kitaifa kutoka zaidi ya nchi 130.

XS
SM
MD
LG