Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Julai 27, 2024 Local time: 09:13

AU yaomba wanajeshi zaidi ili kuwashinda al-Shabab


Majeshi ya Umoja wa Afrika nchini Somalia
Majeshi ya Umoja wa Afrika nchini Somalia

Mkuu wa kikosi cha Umoja wa Afrika Somalia, AMISOM, ametaka kuongezwa wanajeshi ili kusaidia ulinzi wa wanajeshi wa nchi hiyo katika sehemu zilizo kombolewa kutoka kwa al-Shabab, akisema jeshi la Somalia halina uwezo wa kizisimamia sehemu hizo. kama inavyotegemewa.

Ombi hilo la Francisco Caetano Madeira la kuongezwa idadi isiyojulikana ya wanajeshi wa AMISOM limetolewa wakati kukiwa na wasiwasi kuwa jeshi la Somalia halitokuwa tayari kuchukua jukumu hilo la ulinzi, wakati wanajeshi 22,000 wa AMISOM wanapojitayarisha kuondoka Somalia ifikapo 2020.

Al-Shabab imeendelea kufanya mashambulizi ya kikatili katika mji mkuu wa Somalia, Mogadishu na sehemu nyingine. Mashambulizi yao katika vituo vya kijeshi katika miaka miwili iliopita imepunguza kasi ya AMISOM na Somalia katika kupambana na kundi hilo.

Marekani yatoa tahadhari pia

Kauli ya Madeira ameitoa siku hiyo hiyo wakati mkuu wa kikosi maalum cha Jeshi la Marekani Afrika (AFRICOM) alipotoa tahadhari kwa Kamati ya Huduma za Kijeshi ya Baraza la Seneti huko Washington.

Majeshi ya Umoja wa Afrika (AMISOM) yataanza kuondoka Somalia kuanzia 2018, “ na kama yataondolewa kabla ya Somalia kuweza kuwa na uwezo wa majeshi yake yenyewe, sehemu kubwa ya Somalia inahatari ya kuangukia katika mikono ya al-Shabab au pengine kuwepo uwezekano wa kuwafanya ISIS kuwa na sehemu ya maficho yenye nguvu nchini,” amesema Kamanda Jenerali Thomas Waldhauser.

Baada ya muongo mmoja huko Somalia, nchi ambazo ziko katika eneo hilo zenye kuchangia vikosi vyake katika jeshi la AU zimeanza kuelemewa, Waldhauser amesema.

Tishio la wapiganaji wa IS

Wapiganaji wenye mafungamano na kikundi cha Islamic State tayari ni tishio la ugaidi lililozuka hivi karibuni katika nchi hiyo ya Pembe ya Afrika baada ya watu hao kujitenga na wapiganaji wa al-Shabab mwaka 2015.

Jeshi la Marekani linasemekana linataka kuchukua jukumu kubwa zaidi Somalia kwa ajili ya kupambana na ugaidi, lakini hilo linaweza kuhusisha mashambulizi ya angani, ukiwemo utumiaji wa droni zinazotumiwa kwa mashambulizi, na kuongeza msaada wa majeshi maalumu kwa ajili ya kuvisaidia vikosi vya Somalia.

Rais mpya wa Somalia, mwenye uraia pacha wa Marekani na Somalia Mohamed Abdullahi Mohamed, alichukuwa madaraka mwezi uliopita wakati serikali kuu ikiwa imedhoofika na anajaribu kuongeza mamlaka yake katika maeneo mengine ya nchi hiyo.

Wakati wa ziara yake Somalia wiki hii, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesisitiza haja ya kuwepo msaada zaidi kwa majeshi ya Umoja wa Afrika ambao hawana vifaa vya kutosha baada ya mfadhili wake mkubwa , Umoja wa Ulaya, mwaka jana kupunguza msaada kwa asilimia 20.

XS
SM
MD
LG