Fikiria magari yanayopita, mavazi ya kuvutia na vizuizi vya usalama vilivyowekwa njiani wakati wafuasi wa Trump waliojawa na furaha wakimiminika Washington kwa shangwe kubwa kusheherekea kuapishwa kwake kuwa rais wa 45.
Pia wapinzani wa Trump wanategemewa kuandamana kwa nguvu zote kabla, wakati na baada ya kuapishwa Ijumaa.
Kura za maoni zinaonyesha changamoto mbalimbali kubwa zilizojitokeza wakati akijitayarisha kuchukua madaraka. Tafiti nyingine mpya zilizofanywa na mashirika ya habari CNN/ORC na gazeti la The Washington Post na ABC zinathibitisha kukubalika kwa Trump kumeshuka chini ya asilimia 40, ikimfanya awe ni rais aliyepoteza umaarufu wakati anachukua hatamu za uongozi baada ya miaka mingi kupita ambapo rais aliwahi kupoteza umaarufu.
Lakini kwa Obama ni kinyume cha hivyo, kwani wakati anachukua madaraka alikuwa anakubalika kwa asilimia 79 na George W. Bush alipoingia ikulu ya White House alikuwa anakubalika kwa asilimia 62 ambayo ilikuwa ni tathmini nzuri.
Katika ujumbe wake wa Twitter, Trump alikuwa mwepesi kusema kuwa tafiti hiyo ilikuwa “imechakachuliwa,” na kwamba ni tathmini hizo hizo ndizo zilizo “danganya” wakati wa uchaguzi.
Obama bado maarufu
Kwa kumlinganisha na Trump, Rais Obama anakubalika kwa asilimia 58 katika utafiti uliofanywa hivi karibuni na kkituo cha ukusanyaji maoni cha Gallup Poll, sababu inayoendelea kuwafanya wafuasi wa chama cha Demokratik kuona fahari kubwa na kujivunia.
Obama katika wiki zake za mwisho ameelezea mambo chanya yaliyotokea w akiwa Ikulu ya White House. Hii ni pamoja na kutoa muhtasari wa kumbukumbu yake katika hotuba ya kuwaaga wafuasi wake wiki iliyopita huko Chicago.
“Kwa wale wenzetu waliokuwa na bahati ya kuwa ni sehemu ya kazi tulioifanya na kuona hatima ya uongozi huu, nataka niwaambie hili ni jambo la kututia nguvu na kutuhamasisha. Na mara nyingi imani zenu juu ya nchi yenu na wamarekani wenzenu inathibisha hayo,” amesema Obama.
Mji wakabiliwa na mabadiliko
Katika jiji la Washington, utamaduni uliopo wa kujitayarisha kuapishwa kwa Trump umekuwa ukiendelea vizuri, kwa ukamilifu na majaribio yanafanyika katika kula kiapo ambapo tukio hilo litafanyika kwenye ngazi za bunge la Marekani.
Kwenye mkutano wa waandishi wa habari wiki iliyopita, Trump aliahidi kuwa siku ya kuapishwa kwake itakuwa ni kumbukumbu kubwa. “Januari 20 itakuwa ni kitu cha tunu sana na kizuri. Nafikiri tutapokea makundi makubwa ya watu kwa sababu tuna wafuasi wengi. Ni harakati ambazo kwa kweli dunia haijawahi kushuhudia.”
Wanaoandaa hafla hii wanategemea watu 800,000 watajitokeza katika kuapishwa kwa rais nakutembea kuelekea Pennslyvania Avenue, na kukadiria kuwa na umati sawa na ule uliojitokeza wakati Obama alipokuwa anaapishwa miaka minne iliyopita.
Lakini pamoja na hayo itakuwa ni idadi pungufu ukillinganisha na watu milioni1.8 waliojitokeza kushuhudia rais wa kwanza mweusi Marekani akiapishwa mwaka 2009.
Mpasuko wa kisiasa wajitokeza
Kuapishwa kwa Trump Ijumaa tayari kumezua mzozo wa wanaompinga, kati yao ni wale wanaokataa mipango yake ya kuzuia wahamiaji na kuifuta sheria ya afya aliyoipitisha Obama inayojulikana kama Affordable Care Act.
Pia zaidi ya wawakilishi 50 katika bunge la Marekani wa Chama cha Demokratik wameamua kususia sherehe hizo, kutokana na malumbano yaliyojiri kati ya Trump na Mwakilishi na gwiji wa kupigania haki za wananchi, John Lewis, ambaye ni mdemokratik anayewakilisha Georgia.
Wakati Trump anajitayarisha kuchukua madaraka, anakabiliwa na changamoto nyingi katika hatua za kuliunganisha taifa, kwa mujibu wa mchambuzi wa kisiasa, Michael Barone ambaye yuko kwenye taasisi ya American Enterprise.
Vyombo vya habari na Twitter
Trump ameonyesha kutofurahishwa kwake na vyombo ya habari. Katika mkutano na waandishi wa habari wiki iliyopita alikataa kumtambua mwandishi wa CNN, akiwa amekasirishwa na shirika hilo baada ya kuripoti madai ya kuwa Russia ilikuwa inafanya jaribio kukusanya taarifa za kashfa dhidi ya Trump ili waweze kumdhibiti.
“Hapana, sio wewe, Sio wewe. Shirika lako ni ovu,” Trump alimwambia mwandishi huyo wakati akiendelea kusisitiza kwamba alikuwa na haki ya kuuliza swali.
Mashaka ya Trump juu ya vyombo vya habari na kutegemea kwake kutumia Twitter kama ndio njia kuu ya kuwasiliana na wananchi imebainisha hali mpya inayoikabili Washington, amesema mhariri Tom DeFrank anayechangia makala katika jarida la National Journal.
Japokuwa tathmini ya kukubalika kwake iko chini, Trump bado anaamini anaendelea kukubalika na chama chake, kwa mujibu wa mchambuz, Larry Sabato wa chuo kikuu cha Virginia.
“Kama kawaida, kama tulivyoona wakati wa kampeni, wafuasi wa Trump wanaamini kitu chochote anachosema. Na kama hawaamini, hawajali.” Sabato aliiambia VOA kwa njia ya Skype.
Mabadiliko hayo
Utaratibu wa Trump wa mawasiliano na baraza lake la mawaziri umeonyesha tofauti kubwa ya njia ya mawasiliano na rais anaeachia madarakani.