Rais wa Marekani Barack Obama anawahakikishia wamarekani kufuatia mashambulizi ambayo yamefanyika siku chache zilizopita kwenye ardhi ya Marekani, akisema idara ya polisi na mawakala wa kupambana na ugaidi wapo kazini na amewasihi raia kutoingiwa na khofu.
Akizungumza kutoka New York, mahala ambapo anahudhuria kikao cha mkutano mkuu wa Umoja wa Mataifa, Obama alisema katika wakati kama huu ni muhimu kukumbuka kile ambacho magaidi na ghasia za wenye msimamo mkali wanajaribu kukamilisha.
Rais Obama alisema wataalamu wa kupambana na ugaidi na idara za usalama kwenye kila hatua wanafanya kazi usiku na mchana kuzuia mashambulizi ya ugaidi na wamezuia mashambulizi mengi na kuokoa maisha ya watu wengi. Alisema Marekani inaendelea kuongoza ushirika duniani wa kupambana na kundi la wanamgambo wa Islamic State ambalo limefanya mashambulizi mengi kwa kutumia mtandao.
Majibu ya Rais Obama yalifuatia mashambulizi ya mabomu katika majimbo ya New York na New Jersey siku ya Jumamosi pamoja na shambulizi la uchomaji kisu katika jimbo la Minnesota.