Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 00:51

Nigeria: Changamoto zasababisha muda wa kupiga kura kuongezewa katika baadhi ya maeneo


Magazeti nchini Nigeria.
Magazeti nchini Nigeria.

Raia wa Nigeria walikuwa bado wakipiga kura Jumapili katika baadhi ya maeneo ya nchi baada ya hitilafu kuwazuia kufanya hivyo siku ya Jumamosi, hata ingawa tume ya uchaguzi ilisema ingeanza kutangaza matokeo ya uchaguzi huo wa kitaifa kuanzia saa kumi na mbili jioni saa za Nigeria.

Shughuli ya kuhesabu kura ilikuwa ikiendelea katika maeneo mbalimbali kufuatia zoezi la kupiga kura katika uchaguzi wa rais na bunge wa nchi hiyo ya Afrika Magharibi inayouza mafuta mengi nje ya nchi, huku matokeo ya mwisho yakitarajiwa ndani ya siku tano.

Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi, Mahmood Yakubu, aliambia kikao cha wanahabari katika mji mkuu Abuja kwamba matokeo yaliyokusanywa kutoka kwa majimbo machache kati ya majimbo 36 ya Nigeria yatatangazwa kuanzia Jumapili jioni.

Kinyang'anyiro cha kumrithi Rais Muhammadu Buhari kilitarajiwa kuwa na ushindani mkubwa zaidi katika historia ya Nigeria, huku wagombea kutoka vyama viwili ambavyo vimepishana madaraka tangu kumalizika kwa utawala wa jeshi mwaka 1999, wakikabiliwa na changamoto kubwa isiyo ya kawaida kutoka kwa mgombea wa chama kidogo maarufu miongoni mwa wapiga kura vijana.

Upigaji kura pia ulitarajiwa kuendelea katika baadhi ya maeneo ya kaskazini mashariki mwa jimbo la Borno baada ya mashine za kupiga kura kushindwa kufanya kazi.

Haikuwa bayana ni wangapi kati ya wapiga kura milioni 93 waliojiandikisha nchini Nigeria, ambao hawakuweza kupiga kura siku ya Jumamosi.

Katika maeneo mengi ya nchi yenye watu milioni 200, upigaji kura ulifanyika bila matatizo, licha ya matukio ya hapa na pale ya hli ya sintofahamu.

Kulikuwa na ripoti za ghasia katika jimbo la kaskazini la Kano siku ya Jumapili, ambapo kundi lililojihami lilishambulia kituo cha kuhesabia kura katika mji wa Takai, kabla ya vikosi vya usalama kufika, alisema Rakiya Muhammad, mwangalizi wa uchaguzi ambaye alishuhudia tukio hilo.

XS
SM
MD
LG