Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 18:47

Niger kutangaza matokeo ya uchaguzi wa Rais


Mwanamke mmoja wa Niger akipiga kura katika kituo cha Niamey, March 12, 2011
Mwanamke mmoja wa Niger akipiga kura katika kituo cha Niamey, March 12, 2011

Afisa mwenye cheo cha juu nchini Niger anasema matokeo ya duru ya pili ya uchaguzi wa kiti cha Rais nchini humo yatatangazwa leo,Jumatatu.

Raia wa Niger walipiga kura Jumamosi katika uchaguzi unaotazamiwa kuirudisha Niger katika utawala wa kiraia, zaidi ya mwaka mmoja baada ya jeshi kumuondoa madarakani Rais Mamadou Tandja.

Kiongozi wa upinzani wa muda mrefu Mahamadou Issoufou anatarajiwa kumshinda mshirika wa bwana Tandja, Waziri Mkuu wa zamani Seini Oumarou. Issoufou alishinda duru ya kwanza ya uchaguzi wa mwezi Januari kwa asilimia 36 ya kura, na baadae akaungwa mkono na wagombea kadhaa wa upinzani.

Watu milioni 6.7 walipiga kura katika duru ya pili ya uchaguzi. Mwenyekiti wa tume ya uchaguzi nchini Niger, Abdourahamane Ghousmane, alisema Jumapili kwamba wapiga kura waliojitokeza walikuwa kati ya asilimia 35 na 40.Jeshi lilimuondoa madarakani Rais Tandja mwezi Februari mwaka 2010 baada ya kulazimisha mabadiliko ya katiba na kujiongezea muda wa kutawala na mamlaka.

Kiongozi wa kijeshi Salou Djibo alisema upigaji kura wa Jumamosi uliashiria siku nzuri kwa Niger. Alisema ikiwa uchaguzi unafanikiwa, Niger itaingia katika mfumo wa demokrasia ambayo inaweza kuwa mfano kwa bara la Afrika.

Katiba mpya iliyopitishwa katika kura ya maoni Octoba mwaka jana, inalipa jeshi nafasi hadi April 6 kuirudisha Niger kwenye utawala wa kiraia.
Taifa hilo la Afrika Magharibi lina historia ndefu ya kuwa na mapinduzi na ghasia tangu ipate uhuru kutoka kwa mkoloni Ufaransa mwaka 1960.

Niger ina utajiri mkubwa wa madini ya uranium lakini ni moja ya nchi maskini sana duniani. Miongoni mwa matatizo mengine, nchi hiyo inakabiliwa na ukame, idadi kubwa ya watu wasio na ajira na ugaidi kutoka al-Qaida, tawi la Afrika kaskazini.















XS
SM
MD
LG