Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 13:59

Myanmar yadai ukosoaji wa UN ni hasi


Mtoto ambaye amechoka kwa safari ndefu ya kukimbia mauaji huko Myanmar akiwa anasubiri kupita mpakani Bangladesh.
Mtoto ambaye amechoka kwa safari ndefu ya kukimbia mauaji huko Myanmar akiwa anasubiri kupita mpakani Bangladesh.

Myanmar inasema kukosolewa kwake na Umoja wa Mataifa (UN) jinsi ilivyokabiliana na mgogoro wa wakimbizi wa Rohingya inaweza kuathiri vibaya sana mazungumzo yake na jirani yake Bangladesh.

Vyanzo vya habari nchini Myanmar vinasema kuwa mazungumzo hayo ni kuhusu suala la kuwarudisha Warohingya 600,000 waliokimbia huko Bangladesh wakijihami kutokana na ukatili wa jeshi la Myanmar.

Baraza la Usalama la UN lilitoa tamko Jumatatu likieleza “masikitiko yake makubwa” juu ya ripoti ya uvunjifu wa haki za binadamu na unyanyasaji unaofanywa na jeshi la Myanmar katika Jimbo la Rakhine, na kuhimiza serikali kulidhibiti jeshi hilo.

Ofisi ya Aung San Suu Kyi, ambaye ndiye kiongozi wa Myanmar anayetambulika, imetoa tamko kujibu hoja hiyo Jumatano, ikisema Baraza la Usalama limepuuzia ukweli kuwa “masuala yanayowakabili Myanmar na Bangladesh yanaweza tu kutatuliwa kwa nchi hizo mbili kufanya mazungumzo pamoja.” Tamko hilo limesema mazungumzo na Dhaka “yanaendelea vizuri.”

Mazungumzo hayo yalikuwa yameanza kwa kusuasua kama alivyosema msemaji wa Aung San Suu Kyi alipo liambia gazeti linaloendeshwa na serikali Global New Light la Mynamar wiki iliyopita kuwa Bangladesh ilikuwa inachelewesha mchakato wa kuwarejesha wakimbizi hao mpaka pale itakapopatiwa msaada wa kimataifa.

Msaada huo ni wa thamani ya dola za Kimarekani milioni 400 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya kupanua makazi ya wakimbizi Warohingya wanaoishi katika maeneo yenye msongamano katika kambi hizo katika wilaya ya Cox’s Bazar. Takriban asilimia 60 ya wakimbizi ni watoto.

Wimbi la wakimbizi lilianza baada ya jeshi kuanzisha kampeni ya kuangamiza kabisa vijiji vya Rohingya kwa kujibu mashambulizi yaliyofanywa katika vituo vya polisi Myanmar katika eneo la Rakhine mnamo Agosti iliyopita.

Warohingya walio wachache ambao hawana uraia wameendelea kwa muda mrefu kunyimwa haki zao za msingi katika eneo lenye Wabudha walio wengi Myanmar, ambao wanachukuliwa kama wahamiaji kutoka Bangladesh, ingawa ukweli ni kuwa familia nyingi zimeishi Myanmar kwa vizazi vingi.

Waziri wa Mambo ya Nje Rex Tillerson atafanya ziara yake ya kwanza huko Naypyidaw, mji mkuu wa Myanmar, Novemba 15 ili kutafuta ufumbuzi juu ya mgogoro wa Rohingya na kuonyesha uungaji mkono wa Serikali ya Marekani juu ya mabadililko ya kidemokrasia yanayoendelea Myanmar.

XS
SM
MD
LG