Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 26, 2024 Local time: 05:19

Familia yasema Mkapa alifariki kwa mshtuko wa moyo


Rais wa zamani Tanzania marehemu Benjamin Mkapa.
Rais wa zamani Tanzania marehemu Benjamin Mkapa.

Familia ya rais wa zamani wa Tanzania marehemu Benjamin William Mkapa imesema kuwa kiongozi huyo alikuwa anaugua malaria na hatimaye alifariki kwa mshtuko wa moyo. Matamshi hayo yaliyotolewa katika misa ya maziko ya Mkapa Jumapili mjini Dar es salaam yalilenga kuzima uvumi kwamba alifariki kutokana na virusi vya corona.

Msemaji wa familia William Erio alisema wakati wa sala ya misa iliyotangazwa moja kwa moja katika televisheni kwamba "Mkapa alikutwa na malaria na kulazwa hospitali tangu Jumatano," na kuwa kifo chake kilisababishwa na mshtuko wa moyo akiwa hospitalini hapo.

Msemaji huyo alisema ameona ni vizuri kuweka wazi sababu iliyomwua rais ili kuzima uvumi ambao ulikuwa umeanza kuenea kwamba amefariki kutokana na Covid-19. Mkapa ambaye alikuwa na umri wa miaka 81 alionekana hadharani kwa mara ya mwisho katika mkutano mkuu wa chama tawala cha CCM kilichomteua rais John Magufuli kuwania awamu ya pili ya urais kiasi cha wiki mbili zilizopita.

Sala ya maziko katika uwanja wa taifa ilihudhuriwa na rais John Magufuli pamoja na makamu rais, waziri mkuu na viongozi wengine kadha wa ngazi za juu pamoja na maelfu ya wananchi.

Mkapa ambaye alikuwa rais wa tatu wa Tanzania kati ya 1995 na 2005 atazikwa Jumatano katika kijiji chake Lupaso katika mkoa wa Mtwara.

XS
SM
MD
LG