Mwanasiasa mwenye asili ya kipakistani, Sadiq Khan, anaonekana atakua meya wa kwanza muislamu wa mji mkuu wa Uingereza, London huku kura zikiendelea kuhesabiwa.
Bw Khan, mwenye umri wa miaka 45, ani mbunge na wakili na ni mtoto wa wahamiaji kutoka Pakistani, na ushindi wake unatizamwa kama mabadiliko ya kihistoria.
Waislamu wa Uingereza wanachukulia kushinda au kushindwa kwa Khan ni ishara ya kuongezeka kwa ushawishi wao wa kisiasa katika moja wapo ya taifa kuu la dunia. Mohammed Lalmiah, mmiliki wa mgahawa, aliyestaafu, amiambia Sauti ya Amerika kwamba wakati yeye na Waislamu wengine walipofika mjini London, hakukuwa na msikiti, na kwamba walikuwa wanasali kwenye eneo la chini la nyumba yao.
Lalmiah ana matumaini kwamba Khan akiwa meya itakua rahisi kupata vibali vya kujenga misikiti zaidi na taasisi nyinginezo za kuwahudumia Waislamu wanaoengezeka huko Uingereza.