Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Mei 11, 2024 Local time: 06:15

Makundi yanayo watetea wahamiaji yaandamana Marekani


Waandamanaji wakipinga sera za uhamiaji za Rais Trump, Marekani.
Waandamanaji wakipinga sera za uhamiaji za Rais Trump, Marekani.

Maelfu ya watu wameandamana miji mbalimbali nchini Marekani Jumamosi kupinga msimamo wa Rais Donald Trump ambao hauna uvumilii kabisa katika kukabiliana na wahamiaji haramu jambo ambalo limepelekea watoto kutenganishwa na wazazi wao na kuwekwa katika mahema na vizuizi mbalimbali.

Trump alituma ujumbe wa tweet baadae Jumamosi akisema kuwa sheria za uhamiaji za nchi hii, “ ni za kijinga kuliko zote duniani” na kwamba wahamiaji warejeshwe katika nchi zao bila ya kupewa fursa ya kupitia mchakato wa kisheria kabla ya kuondolewa nchini.

Muungano wa wanaharakati, yakiwemo makundi ambayo yaliandaa maandamano makubwa ya wanawake miaka miwili iliyopita, wamesaidia kuratibu maandamano zaidi ya 600 katika miji mikubwa na midogo, katika mji mkuu wa Marekani, huko Hawaii na Puerto Rico, kadhalika katika daraja la kimataifa kati ya El Paso, Texas na Juarez, Mexico na hata huko Antler, North Dakota, population 27

Waandaaji wanasema waliungwa mkono kwa nguvu zote na akina mama ambao wanapinga sera ya zamani ya utawala wa Trump inayo tenganisha watoto kutoka kwa wazazi wao katika mpaka wa Marekani na Mexico. Wakina mama wa nyumbani kadhaa waliandaa maandamano Jumamosi huko Portland, Oregon.

Mjini Washington, mtoto wa kike wa miaka 12 aitwaye Leah, ambaye wazazi wake ni wahamiaji wasio kuwa na kibali cha kuishi Marekani, alitoa ujumbe wenye hisia kali kwa watoto wote wahamiaji.

“Nataka niwaambie watoto walioko mpakani na nchi nzima wasikate tamaa na wapiganie kuungana na familia zao. Sisi sote ni binadamu na tunastahili kupendwa na kusimamiwa! Sisi ni watoto!” aliuambia umati mkubwa uliokuwa ukimshangilia.

Mchungaji wa ngazi ya juu wa kanisa la The King United Church of Christ, Missouri, Traci Blackmon, aliuambia umati wa waandamanaji mjini Washington, “Tulikuwa katika njia hii siku za nyuma. Lazima tusisahau hili. Lazima tukumbuke siku zote hili sio tu suala la sera salama ya uhamiaji bali ni itikadi ya ubinafsi.”

Kadhalika mjini Washington, Lin-Manuel Miranda, aliye buni muziki wa “Hamilton” aliimba wimbo uliokuwa mahsusi umeandaliwa kuwaliwaza wazazi ambao hawana uwezo wa kuwaimbia watoto wao ambao wamechukuliwa kwa nguvu kutoka mikononi mwao..

Waandamanaji huko mji wa New York, ambako ni nyumbani kwa Trump, walikuwa wakiimba “Hakuna chuki, hakuna vitisho, wahamiaji wanakaribishwa hapa Marekani!” wakiwa katika uwanja wa Manhattan jua likiwa limewaka barabara, kabla ya kuelekea na maandamano kuvuka daraja la Brooklyn kwenda katika moja ya uwanja wa kitongoji cha Brooklyn.

Wakati wakiandamana kuvuka daraja, wengi wao waliimba “Ni aibu.” Madereva wa magari walipiga honi kuunga mkono maandamano hayo.

“Ni muhimu kwa uongozi huu kujua kuwa sera hizi ambazo zinavunja familia – ambazo zinawatendea watu unyama, na kuwachukulia watu hao kama wadudu – sio njia anayotaka Mungu, hizi sio sheria za upendo,” amesema Julie Hoplamazian, Mhubiri wa Kanisa la Episcopal aliyekuwa katika maandamano hayo.

XS
SM
MD
LG