Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 11:25

Majeshi ya Ukrainian, Russia yanapambana kuudhibiti mji wa Kyiv


Majeshi ya Ukraine yakikagua eneo lililoshambuliwa na majeshi ya anga ya Russia, Kyiv, Ukraine, Jumamosi, Feb. 26, 2022. (AP Photo/Vadim Ghirda)
Majeshi ya Ukraine yakikagua eneo lililoshambuliwa na majeshi ya anga ya Russia, Kyiv, Ukraine, Jumamosi, Feb. 26, 2022. (AP Photo/Vadim Ghirda)

Milipuko na milio ya risasi ilikuwa ikisikika Jumamosi katika mji mkuu wa Ukraine, Kyiv, wakati majeshi ya Russia na Ukraine yakipambana kwa ajili ya udhibiti wa mji huo. Maafisa wa Kyiv wametangaza amri ya kutotoka nje kati ya saa kumi na moja jioni mpaka saa mbili asubuhi.

Maafisa wa Ukraine wanawasihi raia wa nchi hiyo kusaidia kuutetea mji wa Kyiv dhidi ya majeshi ya Russia. Kambi ya jeshi katika mji mkuu huo ilishambuliwa lakini jeshi la Ukraine limesema shambulizi hilo lilizimwa

Jengo refu la ghorofa mjini humo liliharibiwa mapema Jumamosi. Waziri wa mambo ya nje wa Ukraine alisema jengo hilo lilipigwa na kombora la Russia. Mfanyakazi wa uokoaji ameliambia shirika la habari la Associated Press kuwa watu sita walijeruhiwa katika shambulizi la kombora. Picha za video zimeonyesha uharibifu mkubwa katika ghorofa za juu za jengo hilo.

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy alitabiri kuwa mashambulizi kwa Kyiv yataongezeka zaidi Jumamosi.

“Kyiv inahitaji usimamizi wa maalum,” alisema. “Hatuwezi kuupoteza mji mkuu.”

Zelenskyy alisema Jumamosi kupitia ujumbe wa Twitter kuwa alikuwa ameongea na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron. “Silaha na vifaa kutoka kwa washirika wetu viko njiani kuelekea Ukraine. Umoja dhidi ya vita unafanya kazi,” alisema katika Twitter.

Waziri wa Ulinzi wa Russia alisema Jumamosi kuwa majeshi ya Russia yameuteka mji wa Melitopol ulioko kusini mashariki mwa Ukraine.

Majeshi ya Russia yanasonga mbele kuelekea Kyiv na miji mikuu mingine ikiwa ni sehemu ya mpango “kuidhoofisha” serikali ya Ukraine ambayo inaonekana imepoteza kasi yake, maafisa wa Marekani na Magharibi wamesema Ijumaa, huku wao na Moscow wakitoa taarifa za operesheni zinazoendelea na mapambano katika eneo hilo.

Afisa wa ngazi ya juu wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani, aliwaelezea waandishi wa habari hali ilivyo kwa sharti la kutotajwa jina ili kuweza kujadili masuala ya kipelelezi, alisema majeshi ya Russia yalikuwa yamerusha zaidi ya makombora 200 tangu kuanza uvamizi huo, mengi kati ya hayo yakilenga jeshi la Ukraine.

“Wanakutana na upinzani zaidi kuliko walivyotarajia,” afisa wa Marekani amesema, akiongeza kwamba majeshi ya Russia yalikuwa bado hayajajizatiti katika mashambulizi ya anga pamoja na kuwa na wingi wa silaha na juhudi za kuangamiza ulinzi wa anga wa Ukraine.

Uwezo wa Ukraine kuamuru na kudhibiti “haujaguswa,” afisa huyo aliongeza.

Mjini Kyiv, Zelenskyy anajitahidi kuliunganisha taifa, akitupilia mbali uzushi kuwa amekimbia nje ya mji huo na kusisitiza yeye na maafisa wengine wa serikali” bado wapo hapa, wanautetea uhuru wetu, taifa letu.”

XS
SM
MD
LG