Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 07:48

Magufuli alenga mhula wa pili, Upinzani wadai kukandamizwa Tanzania


Rais wa Tanzania Dr John Pombe Magufuli
Rais wa Tanzania Dr John Pombe Magufuli

Chama cha CCM, ambacho kimetawala Tanzania tangu nchi hiyo kupata uhuru mwaka 1961, kilishinda uchaguzi wa urais mwaka 2015 kwa asilimia 58 ya kura zilizopigwa.

Rais wa Tanzania John Magufuli, anatarajia kushinda muhula wa pili madarakani katika uchaguzi unaofanyika leo Jumatano, huku makundi ya kutetea haki za binadamu yakimshutumu kwa kukandamiza wanasiasa wa upinzani.

Magufuli anakabiliwa na ushindani mkali kutoka kwa mgombea wa chama cha upinzani cha Chadema, Tundu Lissu.

Lissu alinusurika kifo mwaka 2017 baada ya kupigwa risasi 16.

Miongoni mwa wagombea wengine ni pamoja na aliyekuwa waziri wa mambo ya nje Bernard Membe.

Watu waliompiga risasi Tundu Lisu mwaka 2017 hawajajulikana hadi leo.

Uchumi wa Tanzania umekuwa kwa kiasi cha asilimia 7 katika kipindi cha miaka 4 iliyopita.

Serikali imewekeza mabilioni ya dola katika ujenzi wa barabara, reli, mabwawa ya kuzalisha umeme na kununua ndege kwa ajili ya shirika la ndege la umma.

Serikali ya Tanzania inatarajia kwamba uchumi wake utakuwa kwa asilimia 5.5 kufikia mwaka 2020 huku sekta ya utalii ikitarajiwa kukua kwa asilimia 2.5.

Magufuli amewaahidi wapiga kura kwamba miradi yake ya miundombinu itachochea ukuaji wa uchumi kwa asilimia 8.

Tayari chama chake cha CCM kina viti 28 vya bunge ambavyo imevipata bila kupingwa, kulingana na taarifa ya tume ya uchaguzi.

Kiongozi wa upinzani Tundu Lissu amekuwa akikosoa namna rais Magufuli anasimamia uchumi wa Tanzania na ukiukaji wa haki za binadamu, huku akiahidi “kurejesha mfumo wa utawala unaoheshimu haki za binadamu, haki, uhuru wa raia wa Tanzania na kuboresha maendeleo ya kiuchumi kwa kila mtu.”

Chama cha CCM, ambacho kimetawala Tanzania tangu nchi hiyo kupata uhuru mwaka 1961, kilishinda uchaguzi wa urais mwaka 2015 kwa asilimia 58 ya kura zilizopigwa.

Zaidi ya watu milioni 29 wamesajiliwa kupiga kura hii leo.

Tanzania ina jumla ya watu milioni 58.

Wanasiasa wa upinzani na makundi ya kutetea haki za binadamu wamesema kwamba serikali imekuwa ikikandamiza upinzani na kufunga vyombo vya habari, pamoja na kupiga marufuku mikutano ya wanasiasa wa upinzani wakati wa utawala wa muhula wa kwanza wa Magufuli.

Vyama vya kisiasa vimesema kwamba maafisa wa polisi walivuruga mikutano yao wakati wa kampeni na maafisa wa uchaguzi kuwaondoa baadhi ya wagombea wao kutoka katika kinyang’anyiro cha viti vya bunge.

Maafisa serikalini na tume ya uchaguzi wamekuwa wakikanusha madai hayo.

Imetayarishwa na Kennes Bwire, VOA, Washington DC

XS
SM
MD
LG