Kwenye risala yake ya rambirambi, rais Uhuru Kenyatta amesema taifa linaomboleza kufuatia kifo cha gavana Wahome Gakuru, msomi wa masuala ya uchumi aliyefariki Jumanne asubuhi katika ajali ya barabarani.
“Nimepokea kwa huzuni habari kuhusu kifo cha Dr. Wahome Gakuru, nilimfahamu kama mtu aliyekuwa na bidii ya kufanya kazi”, alisema rais Kenyatta.
Gari lake aina ya Mercedes Benz lilipasuka gurudumu wakisafiri kutoka Nyeri kwenda Nairobi alikotarajiwa kufanya mahojiano na kituo kimoja cha televisheni.
Mlinzi wa gavana huyo pamoja na dereva wake walipata majeraha makubwa katika ajali hiyo na baadaye kupelekwa hospitali.
Gavana mwingine wa jimbo la Nyeri Nderitu Gachagua alifariki Februari mwaka huu baada ya kuugua saratani, na sasa taarifa kuhusu kifo cha mrithi wake gavana Gakuru kimewashtua wakenya wengi.
Risala za rambi rambi zimepokeleza kutoka kwa watu wa tabaka mbali mbali na mashirika tofauti kuelezea huzuni kubwa iliyokumba familia ya marehemu.
Kutokana na kisomo chake katika Nyanja ya uchumi Gakuru alipigiwa kura nyingi zaidi na kushinda kiti cha ugavana mwezi Agosti, baada ya kueneza sera yake ya kuimarisha uchumu katika jimbo lake na Kenya kwa jumla.
Gavana Gakuru alisomea vyuo vikuu vya Willamette na Arizona nchini Marekani hadi mwaka wa 2004.
Kwa zaidi ya miaka kumi aliongoza taasisi na mshirika mbali mbali barani Afrika na kufanya kazi kama mtaalamu wa masual ya biashara na uchumi.
-Imeandikwa na Josphat Kioko