Baada ya kujitenga na Sudan, vinu vingi vya mafuta vilibaki upande wa Sudan kusini, lakini kufikia sasa taifa hilo halijaweza kufadhili au hata kuweka wafanyakazi ili kuendeleza shughuli hiyo. Sudan kusini inasemekana kuwa na thuluthi moja ya mafuta ghafi kwenye mataifa yalioko chini ya jangwa la Sahara, wakati ikizalisha takriban mapipa blioni 3.5 ya mafuta kila mwaka.
Hata hivyo inasemekana kuwa asilimia 90 ya mafuta na gesi haijaguswa ingawa hivi karibuni serikali imesema kuwa itaanza kutoa zabuni kwa makampuni ya kigeni ili kuongeza uzalishaji na mapato kwa serikali.
Vinu vingi vya mafuta viliharibiwa wakati wa vita vya wenyewe kwa wenyewe ambapo uzalishaji wa mafuta wa kila siku ulishuka kutoka mapipa 350,000 kwa siku hadi 150,000. Kwa sasa taifa hilo linategemea wataalam kutoka China na Malaysia kuchimba mafuta yake yanayosafishiwa Sudan na kisha kuuzwa kwenye soko la kimataifa.