Maafisa wa usalama nchini Yemen wamesema kuwa wameukamata tena mji wa kusini wa Mukalla siku moja baada ya ripoti kutolewa kuwa wapiganaji wa Yemen waliuwa zaidi ya wanamgambo 800 wa Al-Qaeda katika shambulizi moja.
Vikosi vya Yemen vimeingia Mukalla Jumatatu baada ya siku mbili za mashambulizi makali ya anga kwenye mji huo wa bandari ulioko kwenye Peninsula ya kiarabu na ambao umeshikiliwa na Al-Qaeda kwa kipindi cha mwaka mmoja uliopita.
Jumatatu muungano unaoongozwa na Saudi Arabia nchini Yemen umedai kuuwa zaidi ya wapiganaji 800 wa kundi la Al-Qaeda ingawa hilo halijathibitishwa na vyanzo huru.
Uongozi wa muungano huo umesema kuwa viongozi wa Al-Qaeda ni miongoni mwa waliouwawa. Muungano huo pia umesema kuwa unakusudia kuruhusu misaada ya kibinadamu kufika katika miji ikiwa ni juhudi za kupunguza hali ngumu wanayopitia watu wa Yemen.