Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 10:21

Madaktari Marekani, Uingereza na Ufaransa wanagoma wakitaka nyongeza ya mishahara


Muuguzi akimhudumia mgonjwa wa virusi vya Corona katika chumba cha wagonjwa mahtuti, hospitali ya Timone, mjini Marseile, kusini mwa Ufaransa.
Muuguzi akimhudumia mgonjwa wa virusi vya Corona katika chumba cha wagonjwa mahtuti, hospitali ya Timone, mjini Marseile, kusini mwa Ufaransa.

Uingereza, Ufaransa na Marekani watakabiliwa na migomo zaidi ya wafanyakazi wanaodai nyongeza ya mishahara na hali njema kazini wakati mashauriano na serikali yakifeli.

Nchini Uingereza wafanyakazi wa huduma za afya na usafiri wameahidi kuendeleza mgomo wao baada ya mikutano na mawaziri na viongozi wa vyama vya wafanyakazi kutofikia suluhu.

Nchini Marekani, maelfu ya wauguzi wameingia katika mgomo katika hospitali mbili kubwa huko New York.

Mgomo ulianza Jumatatu baada ya mashauriano kukwama juu ya wafanyakazi na nyongeza ya mishahara kwa karibu miaka mitatu ya janga la virusi vya corona.

Changamoto katika hospitali Marekani

Takriban wauguzi 3,500 katika kituo cha afya cha Montefiore huko Bronx, New York na kiasi cha 3,600 katika hospitali ya Mount Sinai huko Manhattan wako katika mgomo.

Nchini Marekani Hakeem Shula, ni miongoni mwa wauguzi walio katika mgomo kwenye hospitali ya Mount Sinai huko New York. Anasema wauguzi katika hospitali wameungana pamoja ili kusema kwamba wamechoka kunyonywa.

“Tumechoshwa wagonjwa wetu kunyanyaswa na wengi wetu tumechoka kuona hawapati huduma wanazostahili. Tumeingia katika uuguzi kwasababu tunataka kuwahudumia watu, tunawahudumia wao, tunakuja kwa huruma tuliyonayo. Ni vigumu sana kuja hapa hospitali kila siku tukifahamu kwamba hatuna uwezo wa kuwapa huduma za kweli wanazostahili. Hospitali hizi zinaonyesha kwamba wanachojali ni kupata faida. Hawa ni binadamu na wanastahili heshima. Ndiyo maana tuko hapa nje tunagoma, siyo kuhusu fedha. Kwa kweli ni kuhusu kuokoa maisha," anasema Shula.

Baadhi ya huduma zimeahirishwa katika hospitali za kibinafsi

Hospitali binafsi zimeahirisha huduma za upasuaji ambao si wa dharura, na kuyaelekeza magari ya kubeba wagonjwa kwenye vituo vingine vya afya, kuwatoa wafanyakazi wa muda, na kuwapangia kazi wale wa utawala wenye ujuzi wa uuguzi kufanya kazi kwenye wadi li kukabiliana na mgomo unaoendelea.

Nchini Uingereza ambako huduma za afya zinaendeshwa na Unions Unite ya serikali na Unison, wote wanawakilisha wafanyakazi wa afya wamelaani mwelekeo wa serikali.

Onay Kasaba wa Unite amesema serikali ilieleza bayana kwamba inataka kufanya majadiliano ya kuokoa uzalishaji kwa mabadilishano ya kutoa malipo zaidi.

“Tumekuja hapa kwa nia njema, wanachotaka ni kuzungumza kuhusu uzalishaji. Uzalishaji, wakati wanachama wetu wanafanya kazi saa 18 kwa shifti. Unawezaje kuwa na uzalishaji wenye tija, sielewi. Lakini bahati mbaya hivi leo licha ya kufika hapa kwa nia njema, serikali imeshindwa kwa mara nyingine tena kutumia fursa ya kuweka mambo sawa. Kitu gani kitatokea ni kwamba hatua ya mgomo iliyochukuliwa na wafanyakazi wa magari ya wagonjwa ambao ni wanachama wa Unite, nadhani ni muhimu kukumbuka kote katika NHS siyo tu wauguzi kila mtu ambaye anafanya kazi NHS, ni muhimu kwao,” Kasaba anasema.

Unions wamesema watasimamisha mgomo katika wiki chache zijazo kama watapewa suluhisho kwa mgogoro juu ya malipo mwaka huu, wakati serikali inataka kulenga katika nyongeza ya mishahara kwa mwaka ujao wa fedha.

Serikali inadai kwamba mfumuko wa bei kuendana na nyongeza ya mshahara itachochea ongezeko la bei na kusababisha viwango vya riba kupanda na malipo ya nyumba nayo pia yatapanda.

Uhaba wa wafanyakazi wa afya Ufaransa

Kwa Ufaransa kama zilivyo nchi nyingi za Ulaya, inakabiliwa na uhaba wa wafanyakazi wa afya, hasa katika maeneo ya vijijini, huku hospitali nyingi zikiwa zimeelemewa, wazee, idadi kubwa ya madaktari na wauguzi wanaostaafu na mfumo wenye urasimu.

Mapambano katika mfumo wa afya wa Ufaransa kwa hakika utazidi kuwa mbaya kabla ya mambo kuboreka, Rais Emmanuel Macron alikiri Ijumaa, wakati akiahidi kuboresha hali makazini na kuajiri wafanyakazi zaidi wa afya kwa majukumu ya kiutawala.

Rais Macron anasema “kwa hatua zote hizi ambazo tumezijadili, itachukua muongo mzima kuwa na mabadiliko makubwa. Katika miaka ijayo, tutakabiliana na hali ambayo haina mabadiliko makubwa, kwa hakika hali itakuwa mbaya kuhusiana na afya ya watu. Ukifikiria idadi kubwa ya madaktari wetu, wengi wanakaribia umri wa kustaafu.”

Wakati huo huo, Macron alisema, serikali itaongeza uajiri wa wafanyakazi wa afya, na kuwaachia wafanyakazi wa afya kutibu wagonjwa badala ya kufanya majukumu ya kiutawala.

Mbona hospitali zinakabiliwa na changamoto?

Wakosoaji wanasema mfumo umezisukuma hospitali katika mwelekeo wa chini kutokana na idadi kubwa ya kuhudumia wagonjwa wakati gharama zikupunguzwa pamoja na huduma katika maeneo mengine.

Janga la Covid 19 lilikuwa na athari kubwa tayari kwa rasilimali za afya ambazo zilikuwa zimeelemewa sana.

Hospitali nyingi katika majira ya baridi zililazimika kufuta mipango ya upasuaji au kufunga huduma za dharura wakati wa usiku, sambamba na kupanda kwa magonjwa ya kifua na flu ukiongezea na wagonjwa kulazwa hospitali kutokana na Covid katika baadhi ya maeneo.

XS
SM
MD
LG