Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumanne, Machi 19, 2024 Local time: 11:15

Mabalozi wa kiafrika wanazungumzia matamshi ya Trump


Anatolio Ndong Mba, balozi wa Equatorial Guinea katika U.N na mkuu wa kundi la mataifa 54 ya Afrika
Anatolio Ndong Mba, balozi wa Equatorial Guinea katika U.N na mkuu wa kundi la mataifa 54 ya Afrika

Mabalozi wa kiafrika katika Umoja wa Mataifa-UN wamekutana na balozi wa Marekani, Nikki Haley katika taasisi hiyo ya dunia kuzungumzia kuhusu matamshi yaliyotolewa karibuni ya Rais wa Marekani, Donald Trump ambapo alizifanananisha nchi za Afrika na “shimo la choo.”

Anatolio Ndong Mba, balozi wa Equatorial Guinea katika Umoja wa Mataifa na mkuu wa kundi la mataifa 54 ya Afrika amesema Nikki Haley ‘amesikitishwa’ na matokeo ya matamshi hayo.

Wiki iliyopita kundi la mataifa ya Afrika lilisema katika taarifa kwamba matamshi ya Trump yalikuwa ya ‘kijeuri, kibaguzi na kuchukia wageni.’ Kundi hilo limedai msamaha utoletwe na kufutwa kwa kauli hiyo.

Wanadiplomasia kadhaa ambao walihudhuria kikao cha UN wamesema ilipendekezwa wakati wa kikao na Haley kwamba Trump atapeleka ujumbe kwa mkutano wa viongozi wa Afrika unaofanyika Addis Ababa, Ethiopia Januari 28 na 29.

Ndong Mba amesema mkutano na Haley ulikuwa wa ‘kirafiki sana’ na ‘wa uwazi kabisa.’

Rais wa Marekani, Donald Trump
Rais wa Marekani, Donald Trump

Trump aliripotiwa kutoa matamshi hayo huko White House wakati wa mkutano wiki iliyopita kuhusu suala la uhamiaji. Aliripotiwa kuwalinganisha wahamiaji kutoka Haiti, El Salvador na Afrika akifananisha wanatokea kwenye ‘nchi kama shimo la choo.’

Trump na wanasiasa kadhaa ambao walihudhuria mkutano ambako alitoa matamshi hayo waliripoti ameyasema hayo lakini hivi sasa wanakanusha kwamba rais alitoa matamshi hayo.

Wakati huo huo mabalozi 78 wa zamani wa Marekani kwa nchi za Afrika wamepeleka barua White House wakielezea ‘wasi wasi wao mkubwa’ kuhusu matamshi mabaya ya Rais wa Marekani kuhusu bara la Afrika.

“Kama mabalozi wa zamani wa Marekani kwa mataifa 48 ya Afrika, tunaandika kuelezea wasi wasi wetu mkubwa kuhusiana na ripoti juu ya matamshi kuhusu nchi za Afrika na kubainisha umuhimu wa washirika wetu katika mataifa mengi 54 ya Afrika.”

Mabalozi wa kiafrika walioko Washington wanakutana Ijumaa kuamua jinsi ya kujibu matamshi yanayodaiwa yametolewa na Rais Trump.

XS
SM
MD
LG