Amhara imekuwa jimbo lenye machafuko tangu hatua yenye utata iliyochukuliwa na serikali kuu mapema mwaka huu kuvunja jeshi la jimbo na kuliunganisha katika jeshi la taifa au polisi wa jimbo.
Mkuu wa polisi na mkuu wa kitengo cha kuzuia uhalifu katika wilaya ya kusini mwa Amhara ya Dejen waliuawa na dereva moja kujeruhiwa katika shambulio la Jumatatu, serikali ya wilaya ya Dejen imesema katika taarifa kwenye Facebook.
Jana Jumanne, mkuu wa polisi katika mji wa Shewa Robit aliuawa, ofisi ya meya wa mji huo imesema kwenye Facebook, bila kutoa maelezo zaidi.
Maafisa wamesema amri ya kutotoka nje usiku itawekwa kwa muda usiojulikana kuanzia saa kumi na mbili jioni leo Jumatano katika mji wa Shewa Robit, uliopo mashariki mwa wilaya ya Dejen na kwenye umbali wa kilomita 200 kaskazini mashariki mwa mji mkuu Addis Ababa.
Hakuna kundi lililodai kutekeleza mauaji hayo, ambayo yanafuatia mauaji ya mwezi Aprili ya mwanachama mkuu wa chama cha waziri mkuu Abiy Ahmed.
Forum