Shirika la Afya Duniani WHO limetangaza alhamisi kuwa Liberia haina virusi vya Ebola tena baada ya nchi hiyo ya Afrika magharibi kumaliza kipindi cha siku 42 bila ya kuripoti kesi yoyote ya maambukizi mapya.
Mwakilishi wa WHO nchini humo Dakta Alex Gasasira amesema shirika lake linapongeza serikali ya Liberia pamoja na watu wake kwa kudhibiti hali baada ya maambukizi ya Ebola yaliotokea siku za karibuni.
Amesema WHO itaendelea kusaidia Liberia katika juhudi za kuzuia na kushughulikia kesi zitakazojitokeza. Hii ndio mara ya 4 kwa Liberia kutangazwa kutokuwa na virusi vya Ebola tangu ugonjwa huo ulipozuka miaka 2 iliyopita.
Ugonjwa wa Ebola uliuwa zaidi ya watu 11,000 kwenye mataifa matatu ya afrika magharibi kufikia wakati shirika la WHO lilipotangaza kumalizika kwa maambukizi mwisho wa mwaka wa 2015.
-