Chini ya uongozi wa Rais Moon Jae-in, ambaye amekuwa akishawishi kuwepo mazungumzo zaidi na Pyongyang, serikali ya Korea Kusini imetangaza wiki iliyopita mpango wa kupeleka msaada wenye thamani ya Dola za Kimarekani milioni 8 huko Korea Kaskazini kupitia mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa (UN) UNICEF na WFP.
Maafisa huko Seoul wamesema kuwa msaada huo wa kibinadamu utawaletea faraja makundi ya watu wanyonge wakiwemo watoto, wengi wao wanaathiriwa na vikwazo vilivyowekwa dhidi ya Korea Kaskazini.
Kama hili litafanikiwa, itakuwa ni msaada wa kwanza wa serikali hiyo kwenda Korea Kaskazini tangu Disemba 2015. Mtangulizi wake Moon, Park Geun-hye, alisitisha msaada baada ya serikali ya Pyongyang kufanya jaribio la nyuklia mwezi mmoja baadae.
Kutolewa kwa msaada huu wa kibinadamu, wakati ambapo Rais wa Marekani na Kiongozi wa Korea Kaskazini Kim Jong Un wametoa kauli kali za malubano ya kisiasa, imeibua maswali mengi na wasiwasi kuhusu muda ambao Seoul imetangaza kutoa msaada huu.
Baada ya Korea Kaskazini kufanya jaribio kubwa la nyuklia kuliko yote la sita na kuendelea kurusha makombora baadhi ya wachambuzi wanasema msaada huo unaweza kuonekana kuwa unabeza juhudi za kimataifa kuitenga Korea Kaskazini kifedha.