Kimbunga Irene kinapiga mashariki mwa Marekani kwa mvua kubwa na upepo mkali, baada ya kusababisha vifo vya watu wanne. Maafisa wa Marekani wanasema watu watatu wamekufa North Carolina na mmoja katika jimbo la Virginia.
Upepo mkali ukiambatana na mvua kubwa, ukosefu wa umeme imekuwa dalili kuwa hatimaye Irene kimeingia nchi kavu mashariki mwa nchi.
Kimbunga hicho kikali kiliwasili nchi kavu Jumamosi katika jimbo la North Carolina, na kusababisha mafuriko katika mitaa ya miji kadha, kuangusha miti huku kikiwa na upepo wenye kasi ya kilomita 140 kwa saa. Zaidi ya nyumba 630,000 pamoja na biashara hazina umeme katika jimbo la North Carolina.
Kituo cha taifa kinachofuatilia vimbunga kinasema kimbunga hicho kitaendelea kuelekea kaskazini-mashariki na Marekani kwa kasi ya kilomita 24 kwa saa. Wabashiri wa hali ya hewa wanasema kimbunga hicho kitapita eneo la mji mkuu Washington DC majira ya jioni na usiku kucha bila kupungua nguvu.