Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Machi 29, 2024 Local time: 07:56

Kenyatta ashinda uchaguzi wa urais, Raila asusia hafla


Rais Uhuru Kenyatta akihutubia sherehe za Jamhuri Day 2016. .Kenyatta alishinda awamu ya pili ya urais kwa kupata kura milioni 8.2
Rais Uhuru Kenyatta akihutubia sherehe za Jamhuri Day 2016. .Kenyatta alishinda awamu ya pili ya urais kwa kupata kura milioni 8.2

Tume ya uchaguzi na mipaka nchini Kenya, IEBC, Ijumaa usiku ilimtangaza rais Uhuru Kenyatta kuwa mshindi a uchaguzi wa urais uliofanyika siku ya Jumanne.

Kwa mujibu wa tume hiyo, Kenyatta alipata kura milioni 8,196,313 huku mpinzani wake wa karibu, Raila Odinga akizoa kura 6,793,919.

Akizungumza kwenye hafla iliyofanyika katika ukumbi wa Bomas of Kenya, mwenyekiti wa tume hiyo Wafula Chebukati alisema uchaguzi wa mwaka huu ulifanikiwa na kutekelezwa kwa njia ya ustadi.

Muungano wa National Super Alliance (Nasa) ulisusia hafla hiyo baada ya kuwasilisha malalamiko kwa tume hiyo kwamba uchaguzi huo uligubikwa na dosari.

Kenyatta alikuwa anawania muhula wa pili baada ya kumshinda Odinga kwenye uchaguzi wa mwaka wa 2013, ambao mshindi wake aliamriwa na mahakama ya juu.

Akihutubia waliohudhuria kikao hicho, Kenyatta alimshukuru mpinzani wake Raila Odinga, na kutoa wito kwake kujiunga naye kwa ujenzi wa taifa.

"Kama ambavyo nimekuwa nikisema, mashindano ya kisiasa si uadui," alisema.

Alishukuru tume ya IEBC kwa kile alichokiita "kazi nzuri sana."

Wakenya 15,073,602 walipiga kura kwenye uchaguzi huo uliokuwa na ushindani mkubwa amnbapo wagombea kutoka maeneo ya uwakilishi bunge 290 pia waling'ang'ania nyadhifa mbalimbali.

Tangu uchaguzi huo kufanyika, viongozi wa muungano wa NASA, walianza kutoa malalamiko na kushutumu tume hiyo kwa kile ilichokiita "kusimamia zoezi lisilokuwa na maana au ukweli woyote."

Uhuru, mwenye umri wa miaka 56, alifanya kampeni iliyosisitiza miradi aliyoanzisha tangu kuchukua usukani mnamo mwaka wa 2013. Mgombea wake mwenza nalikuwa ni naibu wake wa rais, William Samoei Arap Ruto, mwenye umri wa miaka 50.

Wengi wa waangalizi wa kimataifa walikuwa wamesema kuwa uchaguzi huo ulikuwa wa wazi na wa haki.

Haikujulikana mara moja ni hatua gani Odinga na viongozi wengine wa NASA walinuia kuchukua baada ya tangazo hilo.

XS
SM
MD
LG