Maafisa wa Kenya na Uingereza wamekutana mjini Nairobi kuzungumzia ukame ambao umepelekea maelfu ya Wasomali kukimbilia Kenya kuepuka njaa.
Waziri mkuu wa Kenya Raila Odinga amesema Kenya ingependa mipango ya kulisha watu ifanyike kwenye upande wa Somalia ili kuzuia wimbi la wakimbizi kuingia.
Pia amerudia tena wito wa msaada wa kimataifa ili kusaidia mzozo huo uliosababishwa na ukame.
Kambi zilizojaa kupita kiasi kwenye eno la Dadaab huko Kenya zina idadi ya wakimbizi wapatao laki nne na arobaini ikiwa ni mara nne zaidi ya idadi kambi hizo zinavyotakiwa kuchukua.
Kenya ilikubali Ijumaa kufungua tena kambi yake isiyotumika huko mashariki mwa Dadaab ili kupunguza wimbi hilo.