Upatikanaji viungo

Breaking News
Ijumaa, Aprili 19, 2024 Local time: 07:08

Kenya, Rwanda na DRC zimeunga mkono kura ya kuishutumu Russia, Tanzania, Burundi na Uganda hazikupiga kura


Namna nchi wanachama wa umoja wa mataifa zilivyopiga kura ya kukashifu hatua ya Russia kujitengea kimabavu sehemu 4 za Ukraine, katika kikao cha dharura cha 11 cha umoja wa mataifa Oct. 12, 2022.
Namna nchi wanachama wa umoja wa mataifa zilivyopiga kura ya kukashifu hatua ya Russia kujitengea kimabavu sehemu 4 za Ukraine, katika kikao cha dharura cha 11 cha umoja wa mataifa Oct. 12, 2022.

Idadi kubwa ya nchi wanachama katika Umoja wa Mataifa zimepiga kura ya kuikashifu hatua ya Russia kwa kujiingiza katika mikoa minne ya Ukraine.

Nchi 143 zimepiga kura ya kukemea hatua hiyo kati ya nchi 193 wanachama wa umoja huo.

Nchi tano zimepinga hatua hiyo. Nchi hizo ni Korea Kaskazini, Syria, Belarus, Nicaragua na Russia yenyewe.

Nchi 35 zimesusia kura hiyo.

Kura hiyo imefanyika siku chache baada ya Russia kuanza kurusha makombora kiholela ndani ya Ukraine na kusababisha vifo na uharibifu kwenye mfumo wa umeme.

Bangaldesh, Iraq na Morocco ambazo zilisusia kura ya mwezi Machi ya kulaani uvamizi wa Russia nchini Ukraine, zimepiga kura ya kuunga mkono kuishutumu vikali hatua ya Russia kunyakua sehemu za Ukraine.

Idadi kubwa ya nchi za Amerika, Ulaya, Asia na Afrika zimeunga mkono kura hiyo.

Balozi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa Linda Thomas-Greenfield, ameliambia baraza hilo kabla ya upigaji kura kwamba “Leo ni Russia inaivamia Ukraine, kesho inaweza kuwa nchi nyingine itakayoivamia nyingine. Huenda ikawa ni wewe. Huenda wewe ndiye utakayevamiwa baada ya Ukraine. Utataka baraza hili lifanye nini?”

Russia itawajibishwa

Mwanajeshi wa Russia akiwa vitani katika eneo la Donetsk, Ukraine. May 7, 2022
Mwanajeshi wa Russia akiwa vitani katika eneo la Donetsk, Ukraine. May 7, 2022

Balozi wa Uingereza kwenye Umoja wa Mataifa Barbara Woodward amesema kwamba Russia imeshindwa katika vita hivyo.

“Russia imeshindwa katika mkakati wake wa vita na imeshindwa katika Umoja wa Mataifa”.

Naye balozi wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell amesisitiza kwamba “Russia itawajibishwa. Umoja wa Ulaya utaisaidia Ukraine kwa kila hali hata vita vikichukua muda mrefu zaidi”.

Mwakilishi wa Russia katika Umoja wa Mataifa Vassily Nebenzia amekemea msimamo wa nchi za Magharibi dhidi ya Russia akisema kwamba ni “unafiki mkubwa” huku akitetea hatua ya Russia kutwaa sehemu 4 za Ukraine.

“Mataifa ya magharibi yana maslahi yake ya kieneo na wanajaribu kuihadaa Umoja wa Mataifa kuyaunga mkono,” amesema Nebenzia.

Mataifa ya Afrika 19 yamesusia kura hiyo

Kikao cha viongozi wa Afrika katika umoja wa Afrika (AU) mjini Addis Ababa, Ethiopia, Feb. 5, 2022.
Kikao cha viongozi wa Afrika katika umoja wa Afrika (AU) mjini Addis Ababa, Ethiopia, Feb. 5, 2022.

Miongoni mwa mataifa ya Afrika ambayo yamesusia kura ya Umoja wa Mataifa ni Djibouti ambapo China ina kambi yake ya kijeshi. Nchi hiyo ilipiga kura ya kukemea vita vya Russia nchini Ukraine mwezi Machi na sasa imebadili msimamo.

Afrika Kusini na Ethiopia zimeongoza nchi za Afrika ambazo zimesusia kura hiyo.

Washirika wa muda mrefu wa Russia ambao ni Kazakhstan, Kyrgyzstan, Tajikistan na Uzbekistan nao pia wamesusia kura hiyo.

Nchini wanachama wa Jumuiya ya Afrika mashariki, Kenya, Rwanda na Jamhuri ya kKdemokrasia ya Congo zimepiga kura ya kuishutumu Russia, huku Tanzania, Uganda, Burundi na Sudan Kusini hazikupiga kura kuishutumu Russia.

XS
SM
MD
LG