Upatikanaji viungo

Breaking News
Alhamisi, Machi 28, 2024 Local time: 20:02

Kenya imefilisika, asema mgombea urais Musalia Mudavadi


Musalia Mudavadi, Makamu wa rais wa zamani wa Kenya.
Musalia Mudavadi, Makamu wa rais wa zamani wa Kenya.

Kiongozi wa chama cha Amani National Congress (ANC) na aliyekuwa makamu wa rais wa Kenya Wycliff Musalia Mudavadi, Jumapili alisema kwamba Kenya imefilisika kwa sababu ya usimamizi mbaya na hulka ya serikali kuchukua mikopo ya kimataifa kiholela.

Mudavadi alisema hayo katika ukumbi wa Bomas of Kenya, nje kidogo ya mji wa Naironi, alipozidua rasmi azma yake ya kugombea urais wa Kenya kwenye uchaguzi mkuu wa tarehe 9, mwezi Agosti mwaka huu.

Mwanasiasa huyo alishutumu vikali serikali ya Rais Uhuru Kenyatta kwa “kutowaambia Wakenya ukweli Wkuhusu hali ya uchumi.”

“Kenya imefilisika. Tusidanganyane,” alisema.

Mikopo iliyochukuliwa na serikali hii imewekwa siri na Wakenya wana haki ya kujua ukweli,” aliongeza.

Alisema mikopo ya Kenya inelekea kufika Trilioni tisa huku pato la kitaifa likiwa takriba Trilion 12.

"Na tunaambia kila wakati kwamba tusiyazungumzie mambo hayo," alisema.

China, ambayo imetoa takriban thuluthi moja ya madeni ya nje ya Kenya kwa mwaka wa fedha 2021-22, ndiyo mkopeshaji mkuu wa kigeni baada ya Benki ya Dunia.

Mwaka jana, gazeti la Bloomberg la Marekani lilripoti kwamba Kenya ilipanga kutumia jumla ya shilingi bilioni 117.7 kulipia deni la China katika kipindi hicho, ambapo takriban shilingi bilioni 24.7 ni malipo ya riba kwa mujibu wa nyaraka za bajeti.

Mudavadi hata hivyo alisema serikali haijafichua makubaliano kamili ya malipo ya mikopo hiyo, licha ya kwamba wananchi ndio wanaoigharamia.

"Wakenya sasa wanakabiliwa na mzigo mzito wa kulipa kodi kubwa ambazo zinatozwa kiholela na serikali," alisema Mudavadi huku akishangiliwa na waliohudhuria.

Mudavadi alisema sababu zake za kutaka kuwa rais ni kuikomboa Kenya ambayo imetumbukia “kwenye lindi la ufisadi na madeni.”

Alisema ananuia kuleta mabadiliko kwenye mfumo wa ustawi wa kiuchumi na kuongeza kuwa ana ‘mikono safi’ na maarifa.

Kwa muda sasa, serikali ya Rais Uhuru Kenyatta imekuwa ikikosolewa na baadhi ya wapinzani kwa kuchukua mikopo kutoka taasisi na serikali mbalimbali na kutofichua makubaliano ya malipo ya mikopo hiyo.

"Ninataka kuongoza safari za kurudisha nchi yetu kwenye mkondo uaminifu. Ili kuleta mabadiliko katika ustawi wa kiuchumi, kurejesha uaminifu, kusema ukweli, kufanya kile ninachosema na siyo kuahidi kile ambacho siwezi kufanya," Mudavadi alisema.

Aliongeza: "Nimesafiri na watu waliofanya maovu na wakipewa nafasi ya kujikomboa, bado wanaishia kwenye maovu yao ya zamani,".

Naibu wa Rais Wiliam Ruto, ambaye pia ametangaza azma yakeya kugombea urais, alihudhuria kongamano hilo.

Wengine ambao wametangaza nia yao ya kugombea urais ni kiongozi wa chama cha ODM, raila Odinga, Spika wa bunge la kitaifa Justin Bedan Muturi, Mwenyekiti wa chama cha KANU, Gidion Moi na kiongozi wa chama cha Wiper, Steohen Kalonzo Muyoka.

Mapema Jumapili, Kalonzo na Moi ambao walikuwa wanahudhuria kongamano hilo, waliondoka kwa haraka, baada ya kuambiwa kwamba naibu wa Rais Ruto angehudhuria, kwa mujibu wa baadhi ya waliokuwa kwenye ukumbi huo.

Kiongozi huyo wa ANC pia alipuuzilia mbali uwezekano wa kushirikiana na Odinga katika vuguvugu la kisisa la “Azimio la Umoja” ambalo amekuwa akilipigia upatu.

Mnamo mwaka wa 2019, akiwa katika ziara nchini Marekani, Mudavadi aliiambia idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika kwamba alikuwa tayari kuiongoza Kenya, na kwamba angetumia ujuzi wake kama waziri wa zamani wa fedha kuikombboa nchi hiyo kiuchumi.

“Kenya inaelekea pabaya kiuchumi,” alisema katika mahojiano.

Hata hivyo, wakosoji wa Mudavadi wanasema amewahi kutajwa katika sakata kadhaa za ufisadi, zikiwa ni pamoja na Goldenberg, Anglo Lasing na ile makaburi ya umma.

Akihutubia kongamano hilo, Ruto alisema chama chake cha UDA kitashirikiana na ANC “katika safari ya kuchukua uongozi wa nchi hii.”

XS
SM
MD
LG