Upatikanaji viungo

Breaking News
Jumamosi, Aprili 20, 2024 Local time: 04:19

Jaji mkuu wa Kenya amtaka rais kuvunja bunge


Jaji Mkuu wa Kenya David Maraga (Kulia)
Jaji Mkuu wa Kenya David Maraga (Kulia)

Jaji mkuu wa Kenya David Maraga Jumatatu alimwandikia rasmi rais wa nchi hiyo Uhuru Kenyatta na kumshauri avunje bunge kwa sababu "limeshindwa kutekeleza wajibu wake wa kupitisha sheria" kuhusu kuzingatia usawa wa jinsia katika ugavi wa nafasi za kazi.

Kipengele cha 27 cha katiba ya Kenya ya mwaka 2010 kinaliagiza bunge kupitisha mswada wa sheria unaohakikisha kwamba angalau theluthi moja ya nafasi za ajira zinakwenda kwa jinsia moja - aidha ya kike au ya kiume - na kwamba hakuna jinsia inyofaa kuchukua Zaidi ya theluthi mbili ya nafasi hizo.

Tangu kupitishwa kwa katiba hiyo, ambayo iliipatia bunge miaka mitano kutekeleza wajibu huo, wabunge wamelijadili suala hilo mara kadhaa bila kufikia mwafaka, huku wengine wakikosa kuhudhuria vikao vilivyolijadili, na hivyo kutopigia kura mswada huo.

Tangu wakati huo, makundi na wadau wengine wamewasilisha jumla ya hoja sita mahakani, kuhusu suala hilo.

Mara kwa mara, mahakama ya Kenya imellalamika kwamba bunge halifuati maagizo yako.

Katika barua kwa Rais Kenyatta, Maraga alisema kwamba ingawa hatua hiyo itaigharimu serikali, ni muhimu ichukuliwe, ili kuonyesha kwamba viongozi wa kisiasa wanafuata na kuheshimu katiba ya nchi.

“Ni bora tustahimili uchungu huo kama taifa, ili tujikumbushe kwamba maamuzi tunayoyachukua, yana matokeo yake,” alisema jaji huyo.

Spika wa baraza la wawakilishi la Kenya, Justin Muturi, alipuzilia mbali ushauri huo wa Maraga akisema kwamba hakutilia maanani masuala kadhaa, kabla ya kumwandikia rais Kenyatta.

"Iwapo bunge litavunjwa, katiba inasema ni lazima uchaguzi mkuu ufanyike ndani ya kipindi cha siku sitini. Ningependa Jaji mkuu awaambie Wakenya kama anadhani hilo linawezekana kwa mazingira ya sasa," Muturi alikiambia kituo cha televisheni cha NTV mjini Nairobi Jumatatu usiku.

Iwapo ushauri huo wa Maraga utatekelezwa, atua hiyo ya Jaji Mkuu huenda ikawaacha wabunge wote 418 wa baraza la Wawakilishi na 67 wa baraza la Seneti bila ajira.

Katika siku za nyuma, maspika wa Seneti na baraza la wawakilishi walisema kwamba ni vigumu kutekeleza sheria hiyo bila kuvunja sheria nyingine zinazowapa raia uhuru wa kuwachagua viongozi wanaowataka.

XS
SM
MD
LG