“Jaribio la udukuzi lilifanyika lakini halikufanikiwa,” Mwenyekiti wa Tume Wafula Chebukati aliwaambia waandishi katika mkutano wake na vyombo vya habari Jijini Nairobi. Hata hivyo Chebukati hakutoa maelezo zaidi.
Wakati huohuo Madai ya kiongozi wa upinzani Raila Odinga yalisababisha maandamano katika baadhi ya maeneo ya Nairobi, magharibi ya Jiji la Kisumu na katika mkoa wa Tana River, yakisababisha vifo vya watu wanne waliokuwa wakikabiliana na polisi.
Tume hiyo imesema mpaka Jumatano jioni, Rais Uhuru Kenyatta alikuwa anaongoza kwa asilimia 54 akiwa mbele ya Raila Odinga ambaye amepata asilimia 44.8 ambaye amedai kuwa uchaguzi umekabiliwa na wizi mkubwa wa kura.
Wakenya wanaendelea kusubiri matokeo ya mwisho ya uchaguzi kwa shauku kubwa wakati kuna madai yakuwa kuna wizi wa kura na maandamano ambayo yamepelekea vifo vya watu kadhaa.